Waziri wa Uchukuzi, Mhe. Prof. Makame Mnyaa Mbarawa( Mb) ametoa wito wa kuharakisha matumizi ya mifumo ya kidijitali katika sekta ya bahari ili kuongeza ufanisi na kurahisisha biashara nchini.
Akizungumza Jijini Dar es Salaam, Aprili 20,2026, wakati wa ufunguzi wa semina ya kikanda iliyolenga matumizi ya
IMO Compendium pamoja na utekelezaji wa Maritime Single Window (MSW) na mfumo wa Kidigitali wa Port Community Systems ( PCS), Prof. Mbarawa amesema, hatua hiyo ni muhimu katika kuendana na kasi ya mabadiliko ya teknolojia duniani.
Amesisitiza kuwa Bandari ya Dar es Salaam ina mchango mkubwa, ikihudumia zaidi ya 90% ya biashara ya kimataifa na nchi jirani zisizo na bandari. Maboresho kupitia mradi wa DMGP yameongeza uwezo wa bandari, huku mizigo ikifikia tani milioni 27.7 na muda wa kuhudumia meli kupungua kwa kiasi kikubwa.
Kwa upande wao, Shirika la Uwakala wa Meli (TASAC) na Shirika la Kimataifa la Usafiri wa Majini ( IMO), wameeleza kuwa matumizi ya teknolojia si chaguo tena bali ni lazima kwa bandari za kisasa kwa kufuata miongozo, viwango na taratibu za IMO hasa usalama wa meli, usafirishaji wa mizigo hatarishi na ulinzi wa mazingira baharini.



Serikali imezitaka taasisi zilizoko chini ya Wizara ya Uchukuzi kuangalia namna zinavyoweza kunufaika na uhusiano wa kibiashara katika sekta ya usafirishaji baina ya Tanzania na Misri.
Kauli hiyo imetolewa na Katibu Mkuu wa Wizara ya Uchukuzi Prof.Godius Kahyarara katika kikao kilichokutanisha ujumbe wa Wataalamu wa Wizara ya Uchukuzi ya Jamhuri ya Kiarabu ya Misri na Uongozi wa Wizara ya Uchukuzi ya Tanzania kilichofanyika Makao Makuu ya TPA jijini Dar es Salaam mwishoni mwa juma lililopita. .
Prof. Kahyarara alitaja maeneo kadhaa yenye miradi ya bandari kama Bagamoyo,,Mwanza,Mbamba Bay,Kisiwa Mgao na mradi wa ujenzi wa reli ya kisasa (SGR) itakayorahisisha Uchukuzi wa shehena kutoka bandarini.
Naye Naibu Waziri wa Uchukuzi wa Misri Mhe. Mohamed Fathi alisema ushirikiano baina ya Tanzania na Misri ni wa kihistoria na umekuwa ni ushirikiano katika maeneo mbalimbali ya maendeleo ya kiuchumi.
Akizungumza kwa niaba ya Mkurugenzi Mkuu wa TPA,Mkurugenzi wa Mipango,Ubora na Vihatarishi Dkt.Boniphace Nobeji alisema TPA kupitia Serikali imekuwa ikishirikiana na Misri kwa muda mrefu kwenye eneo la mafunzo kwa watumishi na matarajio ni kuona ushirikiano ukiimarika kwenye eneo la shughuli za kibandari kwa ujumla.
Mara baada ya kikao hicho ,ujumbe huo ulipata fursa ya kufanya ziara katika Bandari ya Dar es Salaam ambako walilakiwa na Mkurugenzi wa Bandari hiyo Bw.Gallus Abed Gallus.



Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari Tanzania (TPA) inashiriki katika maonesho ya Kongamano la Biashara na Uwekezaji la Ziwa Tanganyika (Lake Tanganyika Business and Investment Forum) linalofanyika mkoani Kigoma.
TPA Kupitia jukwaa hilo, inatoa elimu kwa wadau mbalimbali kuhusu huduma za bandari, fursa za uwekezaji katika miundombinu ya bandari, pamoja na nafasi ya bandari katika kurahisisha biashara ya kikanda.
Kongamano hilo limefunguliwa rasmi Aprili 16,2026 na Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Mwigulu Nchemba ambaye katika hotuba yake amesema kuwa jukwaa hilo ni fursa muhimu ya kufungua milango mipya ya ushirikiano wa kiuchumi, kuvutia uwekezaji, na kuimarisha maendeleo endelevu katika ukanda wa Ziwa Tanganyika kwa kuzingatia matumizi bora ya rasilimali na kukuza biashara baina ya nchi wanachama.
Katika kongamano hilo, TPA inashiriki kikamilifu kwa kuwa na banda la maonesho pamoja na uwakilishi ndani ya majadiliano, ikitoa elimu kwa wadau kuhusu majukumu yake ya kusimamia na kuendeleza bandari nchini, miradi ya maboresho ya bandari katika ukanda wa Ziwa Tanganyika, pamoja na mikakati ya kuongeza ufanisi wa Bandari zake.
Ushiriki wa TPA katika jukwaa hilo ni hatua muhimu katika kuimarisha nafasi ya bandari kama mhimili wa biashara na uchumi wa kikanda. Kupitia ushiriki huu, TPA inaendelea kushirikiana na wadau mbalimbali ili kuboresha huduma za bandari na kukuza biashara kati ya nchi zinazozunguka Ziwa Tanganyika.
Kongamano hilo linawakutanisha viongozi wa serikali, wafanyabiashara na wawekezaji kutoka nchi zinazozunguka Ziwa Tanganyika, zikiwemo Burundi, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo ( DRC) na Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kama mwenyeji.



Bandari ya Mtwara imeendelea kupokea wageni mbalimbali ambapo tarehe 16 Aprili, 2026 imepokea ugeni kutoka Kampuni ya Equinor ya nchini Norway wakiongozwa na mwakilishi wao Bw. Noel Cox wakiambatana na mwakilishi kutoka Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC) Bw. Asiad Mrutu, wamefanya ziara ya kutembelea wadau mbalimbali watakaotoa huduma wakati wa utekelezaji wa mradi wa usindikaji gesi asilia (LNG) unaotarajiwa kufanyika katika Mikoa ya Lindi na Mtwara.
Ziara hiyo ilikuwa na lengo la kutathmini na kujiridhisha kuhusu utayari pamoja na uwezo wa Bandari ya Mtwara katika kuhudumia mizigo mbalimbali itakayohitajika katika utekelezaji wa mradi huo mkubwa wa kimkakati mara utakapoanza.
Katika ziara hiyo, wageni walipata fursa ya kuelezwa kuhusu maboresho yaliyofanyika katika Bandari ya Mtwara ikiwa ni pamoja na kuimarishwa kwa miundombinu ya kupakia na kushusha mizigo, kuongezeka kwa ufanisi wa huduma, pamoja na matumizi ya teknolojia za kisasa katika uendeshaji wa shughuli za Bandari. Maboresho hayo yameifanya Bandari ya Mtwara kuwa na uwezo mkubwa zaidi wa kuhudumia mizigo ya aina mbalimbali kwa ufanisi na kwa viwango vinavyokidhi mahitaji ya miradi mikubwa ya kimataifa. Hali hiyo imechochea utayari wa Bandari katika kuhudumia shughuli za mradi mara utakapoanza.
Aidha, Kaimu Meneja wa Bandari ya Mtwara Bw. Mtunze M. Sudi aliwahakikishia wageni hao kuwa Bandari ipo tayari kuhudumia mizigo yao wakati wowote watakapohitaji huduma hiyo. Alisisitiza kuwa uongozi wa Bandari umejipanga kuhakikisha utoaji wa huduma bora za haraka na zenye viwango vya juu ili kusaidia kufanikisha utekelezaji wa mradi huo muhimu kwa maendeleo ya nchi.


Menejimenti ya Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari Tanzania (TPA) imewakutanisha Wadau wa Bandari Kavu katika kikao kilicholenga kujadili changamoto,kupokea mawazo na kubadilisha panapohitajika ili kuongeza ufanisi katika uhudumiaji wa shehena.
Kikao hicho kilichofanyika Aprili 16, 2026 Makao Makuu ya TPA Jijini Dar es Salaam, kiliongozwa na Mkurugenzi wa Masoko na Uhusiano
Dkt.George Fasha ambaye katika hotuba yake ya ufunguzi alisema TPA inatambua umuhimu wa Bandari Kavu katika ufanisi wa shughuli za kibandari nchini.
Aidha Dkt. Fasha aliwataka washiriki wa kikao hicho kujadili kwa uwazi kuhusu maeneo yanayohitaji maboresho na ufanisi katika kuhamisha, kuhifadhi na kushughulikia shehena ndani na nje ya eneo la Bandari Kuu.
Akizungumza kikaoni hapo,Mwenyekiti wa Chama cha Waendesha Bandari Kavu Nchini (CIDAT) Bw.Melickzed Kishange alisema vikao aina hii vina umuhimu mkubwa kwa wadau Bandari Kavu kwani ndio jukwaa litalohadili na kutatua changamoto zitokanazo na shughuli za uhamishaji wa shehena kutoka bandarini.


EN
SW
FR
TPA ChatBot - "Nahodha"