Bandari ya Mtwara imeendelea kupokea wageni mbalimbali ambapo tarehe 30 Aprili, 2026 imepokea ugeni wa wafanyabiashara kutoka Visiwa vya Comoro. Ugeni huo uliongozwa na Balozi wa Comoro Nchini Tanzania Dkt. Ahamada El Badaoui Mohamed.
Lengo la ziara hiyo lilikuwa ni kuwatambulisha rasmi wafanyabiashara hao kwa Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari Tanzania (TPA) pamoja na kuomba ushirikiano katika kuhudumia meli za saruji zitakapowasili katika Bandari ya Mtwara.
Kufuatia ziara hiyo, wafanyabiashara hao wamebainisha kuwa kwa sasa Serikali ya Comoro inaendelea na miradi mbalimbali ya maendeleo ikiwemo ujenzi wa viwanja vya michezo na hospitali jambo linaloongeza mahitaji makubwa ya saruji Nchini Comoro. Aidha, walieleza kuwa kwa sasa wanatumia saruji kutoka Kiwanda cha Dangote ambapo saruji hiyo inasafirishwa kupitia Bandari ya Mtwara kwa zaidi ya tani 10,000 kwa mwezi.
Kutokana na mahitaji hayo, wameomba TPA kuendelea kutoa ushirikiano wa karibu katika kuhakikisha meli zinazobeba saruji zinahudumiwa kwa ufanisi na kwa wakati.
Katika ziara hiyo, wageni hao walipata fursa ya kutembelea miundombinu ya Bandarini hususan katika eneo la gati jipya na la zamani pamoja na ghala linalotumika kuhifadhi saruji ambapo walishuhudia shughuli za upakiaji zikiendelea kutekelezwa.
Kaimu Meneja wa Bandari ya Mtwara Bw. Mtunze M. Sudi alielezea kuwa, maboresho yaliyofanyika katika Bandari ya Mtwara ikiwemo miundombinu na ununuzi wa mitambo imeongeza ufanisi katika utoaji huduma pamoja na utayari wa Bandari kuhudumia mizigo ya aina mbalimbali kwa wakati wote.
Katika hitimisho la ziara hiyo, wageni hao walieleza kuridhishwa na uwezo wa Bandari ya Mtwara baada ya kupata maelezo ya kina na kujionea namna shughuli mbalimbali za bandari zinavyotekelezwa kwa ufanisi mkubwa.


Serikali ya Denmark imeonesha nia ya kuimarisha ushirikiano na Tanzania katika kukuza biashara na uwekezaji kwenye sekta ya uchukuzi kupitia Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari Tanzania (TPA).
Balozi wa Denmark nchini, Mhe. Jesper Kammersgaard, ameeleza Serikali yake kuvutiwa na maendeleo ya Bandari ya Dar es Salaam pamoja na mwelekeo wake wa kimkakati wakati wa kikao na Menejimenti ya TPA kilichofanyika Aprili 30, 2026.
Kwa upande wa TPA, Naibu Mkurugenzi Mkuu, Mha. Dkt. Baraka Mdima amesema uwezo wa kuhudumia shehena umeongezeka maradufu, hali iliyochochea ongezeko la meli bandarini.
TPA pia inaendelea na mipango ya kuendeleza bandari za kimkakati kama Mbegani Bagamoyo na Bandari Kavu ya Kwala ili kuimarisha mtandao wa usafirishaji kwa reli na barabara, na kupunguza msongamano katika Bandari ya Dar es Salaam.


Serikali imesema inalenga kuitumia Bandari Kavu ya Kwala kama kichocheo cha ongezeko la mapato, kupunguza msongamano katika Bandari ya Dar es Salaam na hivyo kuchangia kukuza uchumi wa nchi.
Kauli hiyo imetolewa Aprili 29, 2026 na Katibu Mkuu wa Wizara ya Uchukuzi, Prof. Godius Kahyarara, wakati wa hafla ya kumkabidhi mkandarasi eneo la ujenzi wa Bandari Kavu kwa ajili ya kuhudumia shehena ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC). Hafla hiyo ilifanyika katika Bandari Kavu ya Kwala, iliyopo Mlandizi, Mkoa wa Pwani.
Prof. Kahyarara amesema kuwa uamuzi wa DRC kuanza ujenzi wa bandari yake kavu katika eneo hilo utakuwa chachu kwa nchi nyingine zilizotengewa maeneo katika Kwala kuharakisha ujenzi wa bandari zao kavu, hatua itakayoongeza ufanisi wa huduma za usafirishaji na biashara kikanda.



Serikali ya Belarus imeonesha nia ya kushirikiana na Tanzania kupitia Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari Tanzania (TPA) kuimarisha uchukuzi wa mazao ya kilimo, hususan mbogamboga na nafaka, kupitia Bandari ya Dar es Salaam.
Uwekezaji wa kisasa katika Bandari za Tanzania unaendelea kuvutia mataifa mbalimbali Duniani, huku Bandari ya Bagamoyo na Bandari ya Tanga zikichagizwa kuwa vituo muhimu vya kuhudumia shehena zinazoharibika kwa haraka.
Akizungumza katika kikao kilichofanyika Aprili 29, 2026 Makao Makuu ya TPA jijini Dar es Salaam, Waziri wa Mambo ya Nje wa Belarus, Mhe. Maxima Ryzkhenkov amesema nchi yake imejipanga kuimarisha biashara ya uchukuzi wa mazao yatokanayo na kilimo kupitia Bandari za Tanzania.
Akimwakilisha Mkurugenzi Mkuu, Naibu Mkurugenzi Mkuu wa TPA, Mhandisi Dkt. Baraka Mdima asema Mamlaka ina maeneo kadhaa yanayoweza kutumika kwa ajili ya kuendeleza ushirikiano huo.
Dkt. Mdima ametolea mfano wa Bandari kama ya Tanga, kwamba TPA imepanga kufanya uwekezaji mkubwa wa miundombinu ya kisasa ya kuweza kuhudumia shehena inayoharika haraka.
Naye Balozi wa Jamhuri ya Belarus nchini, Bw. Dzmitry Krasouski amesema wakiwa kama nchi isiyo na Bahari, wamevutiwa mno na uwekezaji mkubwa wa miundombinu uliofanywa katika Bandari ya Dar es Salaam.
Bandari ya Dar es Salaam, ambayo ndio bandari mama, imefanyiwa maboresho makubwa kwa kuongezwa na kurefushwa kwa gati 1-7 ili kupokea meli kubwa zaidi (Panamax/Post-Panamax).
Kina cha maji katika magati kimeongezwa kwa uchimbwa hadi kufikia mita 14.5 ili kuruhusu meli kubwa kuingia bila vikwazo, huku uwezo wa kupokea meli nyingi kwa wakati mmoja ukiongezeka.
Katika bandari hiyo pia, Serikali kupitia TPA kwa kushirikiana na waendeshaji, imewezesha kuongezwa kwa mitambo ya kisasa (RTG cranes, ship-to-shore cranes), kuongezwa eneo la kuhifadhi makontena.
Na kuongezeka kwa kasi ya kushusha na kupakia mizigo kupitia matumizi sahihi ya mifumo ya TEHAMA ya kusimamia mizigo (cargo tracking & clearance) pamoja na kupunguza muda wa kushughulikia mizigo (turnaround time).


Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari Tanzania (TPA), imeendelea kuonesha dhamira yake ya kuimarisha nafasi ya Tanzania katika biashara ya kikanda kwa kushiriki kikamilifu katika mkutano wa Land-Linked Zambia 2026, mjini Lusaka, nchini Zambia.
Ushiriki wa TPA, unalenga moja kwa moja kuongeza shehena ya mizigo inayopitia katika Bandari ya Dar es Salaam, ambayo ni lango kuu la biashara kwa nchi zisizo na Bandari kama Zambia.
Mkutano huo unaleta pamoja wadau mbalimbali wa sekta ya usafirishaji na biashara, wakiwemo Serikali, Mamlaka za Bandari, Waendeshaji wa Reli, na Wawekezaji wa miundombinu.
Kupitia jukwaa hilo, TPA inapata fursa ya kuonesha maboresho yaliyofanyika katika Bandari zake, ikiwa ni pamoja na kuongeza kina cha maji, kupanua magati, na kuboresha mifumo ya kidijitali ya kuhudumia mizigo kwa haraka na kwa ufanisi zaidi.
Kwa Zambia, ambayo uchumi wake unategemea kwa kiasi kikubwa usafirishaji wa madini kama shaba, upatikanaji wa njia ya uhakika na yenye gharama nafuu kwenda baharini ni jambo la msingi.
Hapa ndipo umuhimu wa TAZARA Railway unapojitokeza, ukiunganisha moja kwa moja maeneo ya uzalishaji nchini Zambia na Bandari ya Dar es Salaam. Ushiriki wa TPA katika mkutano huu pia unalenga kuimarisha matumizi ya reli hiyo ili kuongeza ushindani wa ukanda huu wa usafirishaji.
Aidha, mkutano wa Land-Linked Zambia unatoa fursa kwa TPA kujitangaza katika mazingira ya ushindani mkali kutoka bandari nyingine za kikanda kama zile za Msumbiji, Namibia, Afrika Kusini na Angola (Lobito corridor).
Katika ushindani huu, ubora wa huduma, kasi ya upakuaji na upakiaji mizigo, pamoja na gharama za usafirishaji, ni vigezo muhimu vinavyoamua mwelekeo wa wafanyabiashara na wasafirishaji wa mizigo.
Kwa kushiriki katika mkutano huu, TPA inalenga kuvutia wateja zaidi kutoka Zambia na nchi jirani, kuongeza kiwango cha mizigo kinachopitia bandarini, na hivyo kuongeza mapato ya taifa.
Hatua hii pia ina mchango mkubwa katika kukuza ajira, kuimarisha uchumi wa nchi, na kuifanya Tanzania kuwa kitovu muhimu cha biashara na usafirishaji katika ukanda wa Afrika Mashariki na Kusini.
Kwa ujumla, ushiriki wa TPA katika mkutano wa Land-Linked Zambia 2026 ni mkakati mahsusi wa kukuza biashara, kuimarisha ushirikiano wa kikanda, na kuongeza ushindani wa Bandari ya Dar es Salaam katika soko la kimataifa.
Lakini pia ni hatua inayoonesha wazi kuwa Tanzania ipo tayari kunufaika kikamilifu na fursa zinazotokana na dhana ya “land-linked,” kwa kuifanya Zambia na nchi nyingine zisizo na bandari kuwa washirika wakuu wa maendeleo ya uchumi wa taifa.


EN
SW
FR
TPA ChatBot - "Nahodha"