

Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari Tanzania (TPA) imetia saini makubaliano ya taratibu za uendeshaji wa Kawaida (SOPs) zilizotayarishwa kwa ajili ya uhamishaji, uhifadhi na usafirishaji wa shehena kutoka Bandari ya Dar es Salaam hadi Bandari Kavu ya Kwala, iliyopo Wilaya ya Kibaha, Mkoa wa Pwani.
Hafla hiyo ya utiaji saini makubaliano hayo imefanyika Julai 28,2025 Makao Makuu ya TPA jijini Dar es Salaam, ikihusisha Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari Tanzania (TPA), Shirika la Reli Tanzania (TRC) na waendeshaji wa Bandari ya Dar es Salaam, Kampuni za DP World na Tanzania East Africa Gateway Terminal Limited (TEAGTL).
Akizungumza mara baada ya kusainiwa makubaliano hayo yanayoenda kuifungua Bandari ya Dar esSalaam, Mkurugenzi Mkuu wa TPA Bw.Plasduce Mbossa, amesema taratibu hizi zimetayarishwa kwa pamoja na kila Taasisi imeonyeshwa nini inachotakiwa kufanya katika mchakato mzima wa Uchukuzi wa shehena kutoka bandari ya Dar es Salaam.
Aidha Bw.Mbossa amesema makubaliano hayo yatapunguza muda wa uondoshaji mzigo bandarini, msongamano wa magari makubwa, kuongeza ufanisi na kupunguza gharama za uhudumiaji wa shehena.
Naye Mkuu wa Idara ya Utekelezaji wa TEAGTL Bw.Laksiri Noni amepongeza uamuzi wa kushirikisha wadau wote wanaohusika katika mnyororo mzima wa Uchukuzi wa shehena katika makubaliano hayo.

Timu za Mpira wa Wavu ya Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari Tanzania (TPA) Wanaume na Wanawake zimeshiriki ufunguzi wa Ligi ya Mpira wa Wavu Taifa -Tanzania Volleyball National League (TVNL) uliofanyika katika viwanja vya Mwembe Yanga jijini Dar es Salaam.
Kocha wa timu hizo Bw.Willy Barton amesema kuwa vikosi vyake vipo tayari kwa ligi hiyo na kuwahakikishia Menejimenti ya TPA, Mashabiki na Wadau, ushindi katika mechi zote na hatimaye kunyakuwa ubingwa wa michuano hiyo.
Aidha Timu ya Mpira wa wavu wanawake ya TPA, tarehe 26 Julai 2025 itaingia dimbani dhidi ya Jeshi Stars katika mchezo utakaochezwa katika viwanja vya Mwembe Yanga Jijini Dar es Salaam.
Ligi ya Mpira wa Wavu Taifa imeandaliwa na Chama cha mpira wa Wavu Tanzania (TVF) ikishirikisha timu 14 kwa Wanaume na kwa upande wa Wanawake ni timu 7 ambapo ligi hiyo itaanza rasmi kuchezwa tarehe 26 Julai hadi Agosti 1, 2025.

Serikali imetoa wito kwa wananchi, wafanyabiashara, wawekezaji na wadau wote wa sekta ya usafirishaji kushiriki katika hafla ya uzinduzi wa Bandari kavu ya Kwala iliyopo Vigwaza Mkoa wa Pwani, unaotarajiwa kufanywa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, Julai 31,2025.
Akizungumza na Waandishi wa Habari, Julai 25,2025, Makao makuu ya Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari Tanzania ( TPA) Jijini Dar es Salaam, Waziri wa Uchukuzi Mhe. Prof. Makame Mnyaa Mbarawa, amesema hafla ya uzinduzi wa Bandari kavu ya Kwala ni ya kitaifa na itaenda sambamba na uzinduzi wa usafirishaji wa Shehena kwa treni ya SGR Kati ya Dar es Salaam na Dodoma pamoja na upokeaji wa mabehewa ya mizigo ya Treni ya Kawaida (MGR) ambapo mabehewa 50 ni mapya na mabehewa 20 yaliyokarabatiwa kwa ufadhili wa Wakala wa Uwezeshaji wa Ushoroba wa Kati (CCTTFA).
“Rais wetu mpendwa, Dkt. Samia Suluhu Hassan, atazindua rasmi bandari hii muhimu kwa taifa letu, pamoja na huduma za kisasa za usafirishaji wa mizigo. Huu ni uthibitisho wa dhamira ya Serikali ya Awamu ya Sita ya kuimarisha uchumi wa viwanda kupitia miundombinu madhubuti ya uchukuzi,” amesema Mhe. Waziri Prof. Mbarawa.
Mhe. Prof. Mbarawa amesisitiza kuwa bandari hiyo imejengwa kwa lengo mahsusi la kuongeza ufanisi katika kushughulikia shehena zinazowasili katika Bandari ya Dar es Salaam hasa baada ya maboresho makubwa yaliyofanyika kwenye bandari hiyo.
“Kupitia Bandari Kavu ya Kwala, tunategemea ufanisi mkubwa katika kuhudumia shehena. Hii itasaidia kuongeza mapato ya Serikali kutokana na huduma zitolewazo katika Bandari ya Dar es Salaam na Kwala, huku tukipunguza gharama za uendeshaji kwa wafanyabiashara na kuwa kivutio kikubwa kwao kutumia Bandari ya Dar,” amesema Waziri Mbarawa.
Mhe. Waziri ameongeza kuwa hatua hii pia itaongeza ushindani wa Bandari ya Dar es Salaam katika ukanda huu wa Afrika Mashariki, hasa ikizingatiwa kwamba nchi jirani nazo zinawekeza kwa kasi katika bandari zao.
Faida nyingine zilizotajwa na Mhe. Waziri ni pamoja na kupungua kwa msongamano wa magari barabarani hususan Barabara ya Mandela na maeneo ya karibu na Bandari ya Dar es Salaam, kuimarika kwa usalama barabarani na kupungua kwa gharama za matengenezo ya barabara zinazoharibiwa na malori ya mizigo.
Aidha Mhe. Waziri amesisitiza kuwa ujio wa Bandari Kavu ya Kwala umeanza kuleta matumaini kwa wakazi wa Mkoa wa Pwani, ambapo tayari kunashuhudiwa ongezeko la shughuli za kiuchumi, ajira kwa wananchi wa eneo hilo na matarajio ya uwekezaji wa viwanda kutokana na uwepo wa miundombinu madhubuti ya usafirishaji kuelekea Bandari ya Dar es Salaam.
Waziri Prof. Mbarawa pia amewahimiza
wadau hao kuchangamkia fursa zitakazopatikana kupitia huduma za gharama nafuu na ufanisi wa muda mfupi zinazotolewa na Bandari Kavu ya Kwala, treni za kisasa za SGR na mabehewa mapya ya MGR.
Kwa upande wake Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari Tanzania ( TPA) Bw. Plasduce Mbossa, amesema ujenzi wa Bandari Kavu ya Kwala ni sehemu ya mkakati mpana wa Serikali kupunguza msongamano katika Bandari ya Dar es Salaam, huku ikiendelea kuboresha na kupanua miundombinu ya bandari nchini kwa lengo la kuongeza ufanisi na ushindani wa kitaifa na kikanda.
“ Bandari Kavu ya Kwala ni jitihada na mkakati madhubuti wa kitaifa unaolenga kuondoa changamoto sugu ya msongamano wa mizigo Bandarini na maeneo ya barabara ya Mandela Jijini Dar es Salaam.” amesema Bw. Mbossa.

Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi wa Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari Tanzania ( TPA) IJP Mstaafu Balozi Ernest Mangu akiwa na Mkurugenzi Mkuu Bw. Plasduce Mkeli Mbossa, Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Reli Tanzania ( TRC) Mha. Machibya Shiwa na Viongozi wengine, Julai 25,2025, wametembelea Bandari Kavu ya Kwala iliyopo Vigwaza, Kibaha Mkoa wa Pwani, kukagua maandalizi ya uzinduzi wake na usafirishaji wa Shehena kwa treni ya SGR kati ya Dar es Salaam na Dodoma, unaotarajiwa kufanywa na Mhe. Rais wa Jamhuri ya Muungano wake Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan, Julai 31,2025.

Bandari ya Dar es Salaam imevuka lengo la utendaji kwa kuhudumia jumla ya Tani Milioni 27.7 kwa mwaka wa fedha 2024/2025 tofauti ya lengo lililowekwa la kuhudumia Tani Milioni 25.
Mafanikio hayo yamebainishwa na Kaimu Mkurugenzi wa Bandari ya Dar es Salaam Bw. Abed G. Abed, tarehe 23 Julai 2025 wakati akifungua Kikao cha Tatu (3) cha Baraza la Majadiliano kituo cha Bandari ya Dar es Salaam kilichofanyika mjini Bagamoyo Mkoa wa Pwani.
“Ninawapongeza sana kwa ufanisi bora kwa mwaka fedha 2024/2025 tumevuka lengo kwa Tani Milioni 2.7 pia tupo mbele ya ufanisi wa jumla ya Tani Milioni 23.69 kwa Mwaka wa fedha 2023/2024, “ alisema Bw. Abed.
Kaimu Mkurugenzi wa Bandari ya Dar es Salaam amesema mafanikio hayo yametokana na uwekezaji uliofanyika katika Bandari ya Dar es Salaam pamoja ushirikiano wa watendaji wa TPA, wadau mbalimbali na Vyombo vya Usalama waliowezesha shehena kusafirishwa kwa urahisi.
Aidha Bw.Abed amepongeza ushirikiano uliopo kati ya Chama cha Wafanyakazi wa Shughuli za Meli na Bandari Tanzania (DOWUTA) ambao wamewezesha kudumisha amani na utulivu katika Bandari ya Dar es Salaam.