Katika kuadhimisha siku ya Wanawake Duniani, Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari Tanzania (TPA) imetoa msaada wa kadi 400 za bima ya matibabu zenye thamani ya shilingi milioni 20 kwa watoto wenye uhitaji maalum wanaosoma katika Shule Kumi za Wilaya ya Kigamboni jijini Dar es Salaam.
Akizungumza wakati akitoa msaada huo kwa niaba ya wafanyakazi Wanawake wa vituo vya Makao Makuu na Bandari ya Dar es Salaam,Meneja Rasilimali Watu wa Bandari ya Dar es Salaam Bi.Mwajuma Mkonga amesema kutokana na changamoto za matibabu wanazopitia watoto hao TPA imeamua kuwashika mkono kwa kuwalipia bima ya matibabu jumla ya watoto 400 wa shule hiyo iliyopo katika Wilaya ya Kigamboni.
Alisisitiza kuwa mshikamano wa wanawake ni nguzo muhimu katika kuleta mabadiliko chanya katika jamii na kuchangia maendeleo ya Taifa. Aidha, aliwataka wanawake kuendelea kujitokeza katika shughuli za kijamii na kiuchumi ili kuimarisha ustawi wa familia na jamii kwa ujumla


Katika kuelekea kilele cha maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani, Umoja wa Wanawake wa Bandari ya Mtwara umeonesha moyo wa kujali jamii kwa kutoa msaada wa magodoro 13 yenye thamani ya shilingi 2,210,000/= pamoja na mifuko 10 ya sabuni kwa ajili ya kuwasaidia wazee wanaoishi katika mazingira magumu.
Msaada huo umekabidhiwa tarehe 6 Machi, 2026 wakati wa maadhimisho ya Siku ya Wanawake ngazi ya Wilaya yaliyofanyika katika viwanja vya Shule ya Sekondari Naliendele. Hatua hiyo imelenga kuonesha mshikamano na kuwajali wazee wanaohitaji msaada katika jamii.
Mgeni rasmi katika maadhimisho hayo alikuwa Mkuu wa Wilaya ya Mtwara Mheshimiwa Abdallah Mwaipaya ambapo katika hotuba yake aliwahimiza wanawake wa Mtwara kuendelea kuwa na umoja, bidii na uthubutu katika shughuli zao za maendeleo.


Kuelekea kilele cha maadhimisho ya siku ya Wanawake duniani, Wanawake wa Bandari za Ziwa Victoria wakiongozwa na Meneja wa Bandari, Bi. Rosemary Ndesamburo, wameanza maadhimisho hayo kwa kutembelea watoto wenye mazingira magumu katika Kituo cha Fonelisco Children Home Centre kilichopo Wilaya ya Ilemela, Mkoani Mwanza.
Katika ziara hiyo, wanawake hao walipata fursa ya kukaa pamoja na watoto hao, kusikiliza changamoto wanazokabiliana nazo pamoja na kuwapatia mahitaji mbalimbali ikiwa ni ishara ya upendo, mshikamano na kujali watoto wanaohitaji msaada katika jamii.
Hatua hiyo ni sehemu ya kuadhimisha siku hiyo muhimu duniani kwa vitendo, kwa kuonesha mchango wa wanawake katika kujenga jamii yenye huruma, mshikamano na matumaini kwa makundi yenye uhitaji maalum.
Wanawake wa Bandari za Ziwa Victoria wameendelea kuhamasisha jamii kutambua umuhimu wa kusaidiana, kuthaminiana na kushirikiana katika kuleta maendeleo endelevu kwa jamii.

Bandari ya Tanga imehitimisha zoezi la kufanya uchaguzi wa kuchagua Wajumbe Wawakilishi wa Idara na Wajumbe kwa ajili ya Kamati ya Utendaji ya Baraza Dogo la Uchumi la kituo hicho. Pia walichaguliwa Wajumbe wawakilishi kwa ajili ya Baraza Kuu la TPA.
Akiongea katika uchaguzi huo, msimamizi wa uchaguzi kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi , Ajira na Mahusiano, Afisa kazi Mfawidhi wa Mkoa wa Tanga, Bi. Janeth Omolo alisema kuwa, lengo kuu la baraza hilo ni ushirikishwaji wa wafanyakazi katika kutoa maamuzi, kushauri na kutatua changamoto ili kuleta ufanisi mahala pa kazi .
“Mabaraza haya yapo kwa mujibu wa Sheria ya Ajira na Mahusiano Kazini, Sheria za Taasisi za Kazi, Sheria ya Majadiliano ya pamoja, Sheria za Utumishi wa Umma pamoja na Mikataba ya Kimataifa iliyotiwa saini na Tanzania, Sheria zote hizi kwa pamoja zinasimamia mabaraza ya wafanyakazi”. Aliongeza Omolo
Wawakilishi hao waliochaguliwa na idara wanazotoka kwenye mabano ni; Lilian Sauwa (Rasilimali Watu), Innocent Mark ( Fedha), Riziki Mgude (Usaidizi Biashara na Ugavi) na Issa Abdallah ( Ulinzi).
Wengine ni Mathias Lyon (Marine), Joseph Mwambipile na Bernard Malima (Utekelezaji), Twalibu Twalibu (Uhandisi) na Cliff Mkahala (Zimamoto na Uokoaji).
Aidha Baraza la Uchumi liliwachagua Wajumbe Bernard Malima, Mathias Lyon na Twalibu Twalibu kuingia kwenye Kamati ya Utendaji. Pia walichaguliwa Joseph Mwambipile na Lilian Sauwa kuwa Wajumbe wa Baraza Kuu la TPA.
Wakati huo huo Baraza hilo liliwachagua Kelvin Ikunguru kuwa Katibu wa Baraza la Uchumi, Bandari ya Tanga na Mariam Sultan kuwa Naibu Katibu wa Baraza.


Chama cha Wafanyakazi wa Shughuli za Meli na Bandari (DOWUTA) tawi la Makao Makuu wamepongezwa kwa ushindi baada ya uchaguzi Mkuu uliofanyika mwanzoni mwa mwezi Februari, 2026.
Pongezi hizo zimetolewa na Mwenyekiti wa Baraza la Majadiliano (JIC) Naibu Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari Tanzania (TPA) Mha. Dkt. Baraka R. Mdima, tarehe 15 Machi 2026 wakati akifungua kikao cha (60) cha Baraza hilo mjini Bagamoyo Mkoa wa Pwani.
Amesema kuwa DOWUTA ni kiungo katika kuimarisha mahusinao kati ya Wafanyakazi na Menejimenti ya TPA na kuwa chachu ya mafanikio katika kazi.
“Kwa niaba ya Mkurugenzi Mkuu Napenda kuipongeza timu mpya ya Uongozi wa DOWUTA ikiongozwa na Falician Hasunga ikiwa ni sehemu muhimu ya mafanikio ya TPA kwa sababu katika kazi zote tunazofanya mahusiano mazuri kati ya Wafanyakazi na Menejimenti ndio msingi mkubwa wa mafanikio ya kazi.” Amesema Mdima.
Aidha amewahakikishia ushirikinao muda wote katika mambo mbalimbali ili kupata mchango wa kila mmoja na pia kuwa timu moja ambayo kupitia majadiliano italetea matokeo chanya katika kuipeperusha bendera ya TPA.
Pamoja na Mambo mengine Baraza hilo limempongeza Mwenyekiti wa DOWUTA tawi la Makao Makuu aliyemaliza muda wake Bw. Benjamin Kihanga kwa Uongozi uliotukuka na kuwaandaa vema aliowaachia kijiti na kumuomba kuendelea kutoa usaidizi pale utakapohitajika.
Baraza la Majadilioano (JIC ) linafanya kikao cha siku mbili (2), kikilenga kupitia Taarifa ya Utekelezaji wa yatokanayo na kikao cha 59 na kusaini Makubaliano yaliyofikiwa katika kikao cha (60) cha Baraza Dogo la Majadiliano (JIC) Makao Makuu


.
EN
SW
FR
TPA ChatBot - "Nahodha"