Chuo cha Bandari kimeendesha warsha ya siku mbili ya utafiti iliyowakutanisha wanataaluma wa Chuo hicho na wale wa nje kwa lengo la kuimarisha na kuendeleza mipango ya kitafiti ya Chuo hicho.
Katika warsha hiyo jumla ya mapendekezo matatu ya kitafiti yaliwasilishwa na kujadiliwa ili kuyaongezea ubora utakaofikia viwango vya juu vya kitaaluma.

Menejimenti ya Bandari ya Dar es Salaam, Februari 16, 2026 imefanya kikao cha siku moja na wadau mbalimbali wa sekta ya bandari kwa lengo la kujadili masuala muhimu yanayohusu uboreshaji wa huduma na kuongeza ufanisi wa utendaji kazi bandarini.
Kikao hicho kimewaleta pamoja wadau wakuu wanaohusika katika mnyororo wa huduma za bandari, ambapo pamoja na mambo mengine, walijadiliana changamoto zilizopo na kuweka mikakati ya kupata ufumbuzi wa kudumu ili kuongeza kasi ya utoaji huduma na kurahisisha shughuli za biashara.
Baadhi ya wadau waliohudhuria ni pamoja na Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), Shirika la Uwakala wa Meli Tanzania (TASAC), DP World Dar es Salaam LTD, Tanzania East Africa Gateway Terminal (TEGTL), Chama cha Wamiliki wa Malori Tanzania (TATOA),Chama cha Mawakala wa Meli Tanzania (TASAA), Chama cha Wamiliki wa Bandari Kavu Tanzania (CIDAT), Tanzania Customs Agents Association (TACAS), Chama cha Waondoshaji na Wapelekaji Shehena Bandarini na Mipakani Tanzania (TAFFA) pamoja na vyombo vya ulinzi na usalama na taasisi nyinginezo.
Kikao hicho kimeongozwa na Meneja Zimamoto na Usalama, Bw. Mussa Biboze, kwa niaba ya Kaimu Mkurugenzi wa Bandari ya Dar es Salaam, Bw. Abed Gallus Abed.
Menejimenti ya bandari ya Dar es Salaam, imesisitiza umuhimu wa ushirikiano wa karibu kati ya wadau wote ili kuhakikisha huduma zinaboreshwa, muda wa kuhudumia mizigo unapungua na bandari inaendelea kuwa lango kuu la biashara kwa Tanzania na nchi jirani.


Bandari ya Mtwara imepokea jumla ya watumishi wapya 21 waliowasili rasmi Februari 16, 2026, kwa lengo la kuimarisha rasilimali watu na kuongeza ufanisi katika utoaji wa huduma bandarini.
Watumishi hao wametoka katika kada mbalimbali zikiwemo Ubaharia, Ulinzi, Zimamoto na Rasilimaliwatu, hatua inayolenga kuimarisha utendaji kazi katika maeneo muhimu ya uendeshaji wa bandari hiyo.
Akizungumza wakati wa hafla ya mapokezi, Afisa Rasilimaliwatu Mkuu, Bw. Mtunze M. Sudi, aliwapongeza watumishi hao kwa kuanza rasmi safari yao ya Utumishi wa Umma. Aliwasisitiza umuhimu wa uwajibikaji, nidhamu na kufanya kazi kwa weledi ili kufikia malengo ya taasisi.
Aidha, aliwahimiza kuzingatia misingi, kanuni na taratibu za kazi zilizowekwa, kufanya kazi kwa ushirikiano na kuepuka vishawishi vinavyoweza kuathiri maadili ya Utumishi wa Umma. Alieleza kuwa kila mtumishi ana wajibu wa kulinda heshima na hadhi ya taasisi kwa kutekeleza majukumu yake kwa uadilifu na bidii.
Ujio wa watumishi hao unatarajiwa kuongeza tija, kuimarisha utoaji wa huduma kwa wadau mbalimbali na kuendelea kuifanya Bandari ya Mtwara kuwa kitovu muhimu cha biashara katika Ukanda wa Kusini mwa Tanzania pamoja na nchi jirani.
Hatua hii ni sehemu ya jitihada endelevu za TPA katika kuboresha miundombinu na rasilimali watu, ili kuchochea ukuaji wa uchumi wa Taifa kupitia sekta ya bandari.

Waziri Mkuu, Mhe. Dkt. Mwigulu Nchemba, amesema Serikali itaendelea kuiboresha Bandari ya Tanga ili iweze kukidhi ushindani wa kibiashara uliopo katika bandari za mwambao wa Bahari ya Hindi.
Akizungumza Februari 16, 2026 wakati wa ziara yake ya kukagua utendaji kazi wa bandari ya Tanga, Dkt. Nchemba amesema maboresho yanayoendelea ni sehemu ya mkakati wa Serikali kuimarisha sekta ya bandari nchini.
Amesema awamu ya tatu ya maboresho ya Bandari ya Tanga, itahusisha ujenzi wa gati moja mpya ya mita 300 ili kuongeza uwezo wa kuhudumia shehena na meli kubwa zaidi.
Amesema maboresho hayo yanalenga kuimarisha huduma za kibandari na kukidhi mahitaji ya soko, hatua itakayochochea ukuaji wa biashara na uchumi wa Taifa kwa ujumla.
Mapema akimkaribisha Waziri Mkuu kuzungumza na wafanyakazi wa bandari hiyo, Naibu Waziri wa Uchukuzi, Mhe. David Kihenzile, amesema mikakati ya kuendeleza maboresho ya Bandari ya Tanga inaakisi dhamira ya dhati ya Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan, katika kuimarisha sekta ya uchukuzi na kukuza uchumi wa Mkoa wa Tanga na Taifa kwa ujumla.
Kwa upande wake, Naibu Mkurugenzi Mkuu wa TPA, Mha. Dkt. Baraka Mdima, akimwakilisha Mkurugenzi Mkuu Bw. Plasduce Mbossa, aliishukuru Serikali kwa kuendelea kuwekeza katika maboresho ya bandari mbalimbali nchini, zikiwemo bandari za mwambao wa Bahari ya Hindi pamoja na bandari za maziwa, akisisitiza kuwa hatua hiyo itaongeza ufanisi na ushindani katika sekta ya usafirishaji wa mizigo.


Bandari ya Kilwa imeendelea kuwa nguzo kubwa ya kuvutia, kukuza na kuendeleza Sekta ya Utalii Nchini kufuatia kuwasili kwa Meli ya MV LE BELLOT, tarehe 11 Februari, 2026 ikiwa na jumla ya watalii 152 pamoja na wafanyakazi 133.
Ujio wa Meli hiyo unawapa Watalii hao fursa ya kutembelea na kujionea urithi wa kipekee pamoja na vivutio vya kihistoria na kitamaduni vilivyopo Kilwa Kisiwani, eneo lenye umuhimu mkubwa kihistoria.
Watalii hao wanatoka katika Mataifa mbalimbali Duniani ikiwemo Kenya, Marekani, Uingereza, Ujerumani, Ufaransa, Canada, Australia, Uswisi, Hispania, Shelisheli, Norway, Chile na Ubelgiji.
Mchanganyiko huo wa Mataifa unaendelea kuthibitisha hadhi ya Tanzania kama kitovu cha utalii kinachozidi kuvutia Kimataifa. Mafanikio haya yanatokana na juhudi za Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika kuimarisha na kuboresha Sera, Sheria, Miundombinu, Kuendeleza maeneo ya urithi na Kutangaza vivutio vya Utalii nje ya Nchi.
Aidha, juhudi kubwa zimeendelea kutekelezwa na Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari Tanzania katika kuboresha huduma na mazingira ya upokeaji wa meli mbalimbali ikiwemo za Utalii, hatua inayochochea hamasa kwa wadau wa sekta hiyo na kufanya Bandari za Tanzania kuwa chaguo la kuaminika.
Ongezeko la ujio wa Meli za Utalii ni ishara ya mafanikio ya mikakati ya Kitaifa ya kukuza Utalii, Kuongeza mapato ya Nchi, kufungua milango ya fursa za ajira na biashara kwa wananchi wa maeneo husika. Tanzania inaendelea kusonga mbele na kuwa kivutio bora cha Utalii Barani Afrika na Duniani kwa ujumla.
EN
SW
FR
TPA ChatBot - "Nahodha"