Serikali imesisitiza dhamira yake ya kuendelea kuweka mazingira wezeshi kwa sekta binafsi kushiriki kikamilifu katika uboreshaji na uendeshaji wa bandari nchini, hatua inayolenga kuongeza ufanisi wa huduma za bandari na kuchochea ukuaji wa uchumi wa taifa.
Kauli hiyo imetolewa na Waziri wa Uchukuzi, Mhe. Profesa Makame Mnyaa Mbarawa (Mb), tarehe 9 Februari, 2026, wakati wa ziara yake ya kikazi katika Bandari ya Dar es Salaam, ambapo alipata fursa ya kukagua maendeleo ya miundombinu na utendaji wa shughuli mbalimbali za bandari.
Profesa Mbarawa amesema kuwa Serikali inaendelea kushirikiana kwa karibu na sekta binafsi katika kuboresha miundombinu ya bandari, ikiwemo kuimarisha huduma za upakiaji na upakuaji mizigo, kupanua na kuboresha magati, pamoja na kuvutia uwekezaji zaidi wa kimkakati katika sekta ya bandari.
Aidha, Mhe. Waziri amebainisha kuwa ushirikiano huo una lengo la kuongeza ufanisi wa usafirishaji wa mizigo, kupunguza gharama za biashara, na kuifanya Tanzania kuwa kitovu muhimu cha usafirishaji na biashara katika ukanda wa Afrika Mashariki na Kati, hivyo kuongeza mchango wa sekta ya uchukuzi katika kukuza uchumi wa taifa.
Mapema Mhe. Waziri Prof. Mbarawa alipewa maelezo ya kina ya kiutendaji na shughuli za utekelezaji katika Bandari ya Dar es Salaam na Naibu Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari Tanzania (TPA) Mha. Dkt. Baraka Mdima kwa niaba ya Mkurugenzi Mkuu wa TPA, Bw. Plasduce Mkeli Mbossa.


Kampuni ya Lojistiki kutoka nchini Rwanda, African Global Logistics (AGL), imefanya ziara ya kikazi katika Bandari ya Dar es Salaam pamoja na Bandari Kavu za Ihumwa na Isaka, kwa lengo la kutathmini fursa zilizopo za uwekezaji katika sekta ya uchukuzi na lojistiki nchini.
Katika ziara hiyo, ujumbe wa AGL ulipata fursa ya kukutana na Katibu Mkuu wa Wizara ya Uchukuzi, Profesa Godius Kahyarara, ambaye aliukaribisha ujumbe huo na kueleza matarajio ya Serikali kwa kampuni hiyo.
Profesa Kahyarara alisisitiza umuhimu wa mchango wa AGL katika kuongeza tija, ufanisi na ushindani katika Sekta ya Uchukuzi nchini, hususan katika kuimarisha huduma za bandari na usafirishaji wa mizigo.


Naibu Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari Tanzania (TPA), Mha. Dkt. Baraka R. Mdima, amewataka watumishi wapya wa TPA kutokuwa vikwazo katika utoaji wa huduma, bali wawe wawezeshaji wa wananchi na wadau mbalimbali kufanya biashara kwa lengo la kukuza uchumi wa Taifa, Kikanda na wa watu binafsi.
Mha. Dkt. Mdima ametoa wito huo tarehe 5 Februari 2026, alipokuwa akifunga rasmi mafunzo ya awali (Induction Course) ya siku nne kwa watumishi wapya wa TPA, yaliyofanyika katika Ukumbi wa Mikutano wa Jengo la TPA (OSC), jijini Dar es Salaam.
Amesisitiza kuwa TPA ni taasisi inayohudumia wateja wa kitaifa, kikanda na kimataifa, hivyo ni muhimu kwa watumishi wapya kutumia mafunzo waliyopewa kama dira ya kutoa huduma bora, kwa weledi na kwa kuzingatia maslahi mapana ya wateja na uchumi wa nchi kwa ujumla.
“Maamuzi, jitihada na juhudi mtakazoonesha katika utendaji wenu zijenge taswira chanya ya TPA ndani na nje ya Tanzania. Tusiwe vikwazo bali tuwe wawezeshaji wa watu kufanya biashara zao kwa ajili ya maendeleo ya uchumi wa Taifa, Kikanda na watu binafsi,” alisema Mha. Dkt. Mdima.
Aidha, amewasihi watumishi hao wapya kwenda kuwa mabalozi wema wa TPA kwa kutekeleza majukumu yao kwa kushirikiana, kwa uadilifu na weledi, sambamba na kuzingatia malengo na mikakati ambayo TPA imejiwekea ili kuhakikisha taasisi hiyo inafanikiwa katika majukumu yake.
Pia amewahimiza kutobweteka, bali kujenga utamaduni wa kujiendeleza kimasomo, kuuliza maswali na kushirikiana na wafanyakazi wenzao ili kuboresha utoaji wa huduma. Mafunzo hayo yalilenga kuwajengea uelewa kuhusu historia ya TPA na bandari zake, majukumu ya kisheria, Dira na Dhima ya TPA pamoja na Sheria, Kanuni na Miongozo inayosimamia utendaji kazi wa taasisi hiyo.



Shirika la Uwakala wa Meli Tanzania (TASAC), limeridhishwa na kuipongeza Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari Tanzania (TPA) kwa maendeleo ya utekelezaji wa Mradi wa Ujenzi wa Bandari Kavu ya Kurasini.
Mapema leo tarehe 4 Februari, 2026, Mkurugenzi Mkuu wa TASAC
Bw. Mohamed Salum ametembelea mradi huo mkubwa unaotekelezwa na TPA na kuelezea kuridhishwa kwake na hatua iliyofikiwa katika utekelezaji huku akihimiza mradi huo kukamilika kwa wakati ili kuboresha ufanisi wa bandari kwa kuongeza kasi ya huduma.
“Sisi TASAC tumekuja mapema kutoa maoni ya namna ya kuboresha ujenzi wa bandari hii na pia kujipanga kwa ajili ya kufanya ukaguzi. Mradi huu ukikamilika unaweza kuhudumia zaidi ya makasha 700,000, jambo ambalo ni faida kubwa kiuchumi na kutaleta mageuzi makubwa katika uwezo wa bandari yetu, hongera sana TPA.
Mradi huu unalenga kuongeza ufanisi wa kuhudumia makasha katika Bandari ya Dar es Salaam, ambayo kwa sasa inapokea shehena kubwa kutokana na maboresho ya miundombinu na mchango wa sekta binafsi katika kuhudumia meli.
Akiongea kwa niaba ya Mkurugenzi Mkuu Bw. Plasduce Mkeli Mbossa, Kaimu Mkurugenzi wa Bandari ya Dar es Salaam, Bw. Abed G. Abed ameishukuru TASAC kwa kutembelea mradi huo, na kubainisha kwamba eneo hilo lenye ukubwa wa mita za mraba 220,000 lipo katika hatua za mwisho za ukamilikaji.
“Bandari ya Dar es Salaam imefanya vizuri nusu ya Mwaka huu wa Fedha kuhudumia zaidi ya tani milioni 16 za shehena, tunatarajia Mradi huu utakapokamilika Aprili 2026 tutaongeza uwezo wa kupokea makasha mara mbili ya sasa, tutaongeza kasi ya meli kupakia na kuondoka, na kuvutia meli nyingi zaidi kutia nanga bandarini”, amesema Bw. Abed.
Mradi huu utakapokamilika utakuwa umeunganishwa moja kwa moja na barabara, na reli za SGR na MGR, sambamba na uwepo wa taasisi mbalimbali za serikali zinazotoa huduma bandarini ili kuharakisha utoaji huduma.
Ujenzi wa mradi huu unafanyika kwa Awamu mbili, ambapo awamu ya kwanza inatarajiwa kukamilika Aprili 2026 ambapo huduma zitaanza kutolewa mara.


Wanachama wa Chama cha Wafanyakazi wa Shughuli za Meli na Bandari (DOWUTA) Tawi la Bandari ya Dar es Salaam wamemchagua Bw. Mashaka Karume kuwa Mwenyekiti wa Chama hicho, huku Bw. Eliakimu Maluli akishinda nafasi ya Katibu katika Uchaguzi Mkuu wa DOWUTA uliofanyika tarehe 3 Februari 2026 katika viwanja vya Zimamoto na Usalama Bandari ya Dar es Salaam.
Akifungua Mkutano Mkuu wa Chama hicho uliokuwa sambamba na uchaguzi wa viongozi, Kaimu Mkurugenzi wa Bandari ya Dar es Salaam, Bw. Abed G. Abed, kwa niaba ya Mkurugenzi Mkuu wa TPA, Bw. Plasduce Mkeli Mbossa, aliipongeza DOWUTA kwa kudumisha utulivu na mshikamano miongoni mwa wafanyakazi, hali inayochangia kuboreshwa kwa maslahi yao na kuongeza ufanisi kazini.
Bw. Abed alisema kuwa utulivu na moyo wa kujituma wa wafanyakazi, kwa kiasi kikubwa, umechagizwa na mchango wa DOWUTA, hali iliyopelekea kuongezeka kwa ufanisi wa kazi bandarini. Alieleza kuwa katika kipindi cha Julai hadi Desemba mwaka wa fedha 2025/2026, Bandari ya Dar es Salaam imehudumia tani milioni 16.7, ongezeko la tani milioni 3.9 ikilinganishwa na kipindi kama hicho mwaka uliopita.
Aidha, alisema kuwa kwa kasi hiyo ya utendaji, Bandari ya Dar es Salaam inatarajiwa kuhudumia zaidi ya tani milioni 32 ifikapo mwisho wa mwaka wa fedha 2025/2026, kiwango kinachozidi lengo la tani milioni 27.7, mafanikio aliyoyataja kuwa ni matokeo ya ushirikiano mzuri kati ya Menejimenti na DOWUTA.
Katika nafasi nyingine za uongozi, Bi. Sharifa Yahya amechaguliwa kuwa Mweka Hazina, Bw. Shabani Godigodi akishinda nafasi ya Mwakilishi wa Watu Wenye Uhitaji Maalum, huku Bw. David Mtambazi na Bi. Tunu Masenga wakishinda nafasi za Uwakilishi wa Vijana Wanaume na Wanawake mtawalia.
Kwa upande wa Wajumbe Wanawake waliochaguliwa ni Bi. Dainess J. Binemukama, Bi. Theopista W. Millinga, Bi. Chema Y. Mwaduga, Tatu Mandao na Dr. Bertha O. Mushi, huku wajumbe wa idara mbalimbali wakichaguliwa kuwakilisha sekta zao ikiwemo Uhandisi, Utekelezaji, Ulinzi na Zimamoto, Marini, Bandari Ndogo, Rasilimali Watu na Utawala pamoja na Usaidizi wa Biashara, Ugavi, Fedha na Mapato.


EN
SW
FR
TPA ChatBot - "Nahodha"