

Wadau wa sekta ya Uchukuzi wanaoshiriki Mkutano wa pili wa Uchukuzi na Usafirishaji - East Africa Cargo Connect Summit Jijini Dar es Salaam, wametakiwa kuutumia Mkutano huo kuwa na majadiliano yenye faida na yenye kuleta maazimio chanya yatakayoleta mchango mkubwa wenye kuongeza tija na ufanisi katika shughuli za uchukuzi zikiwemo za kibandari.
Kauli hiyo imetolewa tarehe 27 Machi, 2025 na Mkurugenzi wa Masoko na Uhusiano wa TPA Dkt. George Fasha aliyewakilishwa na Afisa Masoko Mkuu Bi. Fatma Adadi Rajab ambaye amesema majadiliano yenye tija ni muhimu kwani mkutano huo unaonyesha nia ya dhati ya Wadau wa Uchukuzi katika kuiboresha sekta hiyo na kuhakikisha utoaji huduma unaendelea kuwa bora zaidi.
Mkutano huo wa siku moja ni jukwaa la kuwakutanisha pamoja Wadau wa sekta ya uchukuzi kwa njia ya maji, anga, reli na barabara, kujadaliana pamoja changamoto zinazowakabili na utatuzi wake pamoja na kufungua fursa mpya za uwekezaji kupitia sekta hiyo na kuikuza zaidi.
Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari Tanzania (TPA) imedhamini Mkutano huo ulioshirikisha Wadau wa Uchukuzi kutoka nchi za Afrika Mashariki, Jumuiya ya maendeleo kusini mwa Afrika ( SADC) na nchi za Afrika magharibi.
Tuzo mbalimbali za umahiri zimetolewa katika Mkutano huo ikiwemo Tuzo ya “The Tanzania Maritime Visionary Leadership Award” iliyotolewa kwa Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari Tanzania ( TPA) Bw. Plasduce Mkeli Mbossa kwa kutambua na kuthamini Uongozi wake wenye maono katika sekta ya uchukuzi wa njia ya maji hapa nchini.

Bandari ya Mtwara imeendelea kupongezwa kwa ufanisi mkubwa wa kuhudumia shehena mbalimbali ikiwemo shehena zenye kemikali.
Pongezi hizo zimetolewa tarehe 25 Machi, 2025 na Mwakilishi wa Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi wa Mamlaka ya Maabara ya Mkemia Mkuu wa Serikali Tanzania Profesa Said Vuai, kufuatia Bodi hiyo kufanya ziara katika Bandari ya Mtwara ambapo imeshuhudia shughuli mbalimbali za utekelezaji zikiendelea.
Kaimu Meneja wa Bandari ya Mtwara Bw. Mtunze Mwarabu Sudi amesema Bandari hiyo imeendelea kushirikiana vema na Ofisi ya Maabara ya Mkemia Mkuu wa Serikali katika kutekeleza shughuli mbalimbali za kuhudumia shehena.

Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma (PIC) imemuelekeza Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi ya Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari Tanzania (TPA) na Menejimenti yake kuendelea kumsimamia ipasavyo Mkandarasi anayetekeleza mradi wa maboresho na upanuzi wa Bandari ya Mwanza Kaskazini ili aweze kukamilisha mradi huo kwa wakati na kwa kiwango kulingana na thamani ya fedha.
Akizungumza Machi 21, 2025 Jijini Mwanza baada ya kutembelea na kukagua mradi huo, Mwenyekiti wa Kamati hiyo Mhe. Augustine Vuma (Mb),amesema kukamilika kwa wakati kwa mradi huo ni hatua muhimu katika kuboresha hali ya usafiri na usafirishaji ndani ya Ziwa Viktoria.
“ Kwa ujumla Sekta ya Bandari Mhe. Rais ametoa fedha nyingi sana na kwa hili tunampongeza sana kwa uamuzi wake huu maana tunaona miradi mingi ya maboresho na ujenzi wa bandari pamoja na ukarabati na ujenzi wa Meli. Kwa ujumla TPA mnafanya kazi nzuri na tunawapongeza kwa mradi huu mzuri na wa kimkakati, muhimu ni usimamizi makini ili mapato yaongezeke na tija ionekane.” Amesema Mhe.Vuma
Pia ameiagiza TPA kuhakikisha inaendeleza ushirikiano na Sekta Binafsi ili kuongeza ufanisi zaidi katika Bandari na kuendelea kuimarisha maeneo ya pembezoni kupitia Bandari.
Akijibu hoja za Wajumbe wa Kamati, Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi ya TPA, Mhe. Balozi na IGP Mstaafu Ernest Mangu, ameishukuru Kamati kwa ziara yao iliyowawezesha kuona mradi wa maboresho na upanuzi wa Bandari ya Mwanza Kaskazini, huku akiihakikishia kamati hiyo kuwa maoni, ushauri na maelekezo waliyoyatoa yatafanyiwa kazi.
Mapema akisoma taarifa ya mradi wa maboresho na upanuzi wa Bandari ya Mwanza Kaskazini mbele ya kamati kwa niaba ya Mkurugenzi Mkuu Bw. Plasduce Mbossa, Naibu Mkurugenzi Mkuu wa TPA Dkt. Baraka Mdima,amesema kukamilika kwa maboresho na upanuzi wa Bandari hiyo kutaenda sambamba na mabadiliko ya kisasa ya Teknolojia katika kuendesha Bandari na kutoa huduma za kiwango cha kisasa zaidi ikiwa ni pamoja na kuongeza tija na ufanisi mkubwa katika kuhudumia Shehena.
Mradi wa maboresho na upanuzi wa Bandari ya Mwanza Kaskazini unagharimu shilingi Bilioni 18.6, ikiwa ni jitihada za Serikali kupitia Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari Tanzania ( TPA) katika kuboresha hali ya usafiri na usafirishaji ndani ya Ziwa Viktoria.

Baraza Kuu la Wafanyakazi wa Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari Tanzania ( TPA) leo tarehe 19 Machi 2025, limefanya kikao chake cha Thelathini na Saba (37) mjini Bagamoyo Mkoa wa Pwani, kinacholenga kujadili na kuthibitisha Mapendekezo ya mpango wa Bajeti ya Mamlaka kwa mwaka wa Fedha 2025/ 2026 pamoja na Kupitia na kuthibitisha Kumbukumbu za Kikao cha Thelathini na Sita (36) kilichofanyika tarehe 2 - 3 Oktoba,2024.
Baraza hilo limeongozwa na Naibu Mkurugenzi Mkuu wa TPA Dkt. Baraka R. Mdima ambapo awali Baraza hilo lilitanguliwa na Kikao cha Kamati ya Utendaji ya Baraza kuu la Wanyakazi kilichoongozwa na Mkurugenzi wa Rasilimaliwatu na Utawala Bw. Mbarikiwa Masinga kwa niaba ya Naibu Mkurugenzi Mkuu wa TPA Dtk. Baraka R. Mdima.

Serikali za Burundi na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo( DRC) zimetoa pongezi kwa Serikali ya awamu ya sita inayoongozwa na Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuweka mikakati madhubuti ya ujenzi na uimarishwaji wa Bandari Kavu ya Kwala iliyopo Mkoani Pwani.
Pongezi hizo zimetolewa tarehe 19 Machi, 2025 na katibu Mkuu wa Wizara ya Uchukuzi kutoka nchini Burundi Bi. Christine Niragira na Mwakilishi wa Wizara ya Uchukuzi ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo ( DRC) Bw. Roger Te- Biasu, baada ya kutembelea Bandari kavu ya Kwala na kukagua maeneo yao yaliyotengwa na Serikali kwa ajili ya kuhudumia Shehena ya mzigo wa Nchi zao unaopita katika Bandari ya Dar es Salaam.
“Tunaipongeza Serikali ya Tanzania na tunampongeza Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kazi nzuri inayofanyika hapa Kwala na kwa kutupatia eneo hili kwani ni njia ya kurahisisha ufanyaji biashara kati ya Tanzania na Burundi nasi kwa sasa tunaendelea kuliendeleza eneo hili haraka”. Amesema Bi. Niragira.
Serikali ya Tanzania imetenga eneo la Hekta 45 kwa DRC na Hekta 10 kwa Jamhuri ya Burundi katika Bandari Kavu ya Kwala, kwa ajili ya kuhudumia Shehena zao zinazopita katika Bandari ya Dar es Salaam.
“ Tumefika hapa Kwala kuona eneo tulilopewa na Serikali ya Tanzania na hakika tumeridhika sana kwani ishirikiano uliopo kati ya Nchi hizi zetu mbili ni kwa maendeleo ya pamoja”. Amesema Bw. Roger Te- Biasu.
Ugeni huo umepokelewa na Mkurugenzi wa Miundombinu ya Uchukuzi Mha. Shomari Shomari kwa niaba ya Katibu Mkuu wa Uchukuzi, ambaye amesema uwepo wa Bandari kavu ya Kwala ni utekelezaji wa vitendo wa maono ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan na kuimarika kwa Bandari kavu hiyo kutafungua Uchumi wa Nchi yetu na kurahisha shughuli za usafirishaji
Kwa upande wake Katibu Mtendaji wa Ushoroba wa Kati (CCTTFA,) Wakili Flory Okandju Okonge, amesema ni faraja kwao kuona nchi saba wanachama aa Ushoroba zinaendelea kunufaika kibiashara na kuendelea kukuza diplomasia ya kiuchumi miongoni mwao kupitia Bandari ya Dar es Salaam na Bandari za Tanzania.
Ujumbe huo umepewa maelezo ya kina kuhusu mradi huo na Meneja Miliki wa TPA Bw. Alexander Ndibalema kwa niaba ya Mkurugenzi Mkuu, ambaye amesema kukamilika na kuanza kutoa huduma kwa Bandari hiyo kutapunguza msongamano Katika Bandari ya Dar es Salaam na kuongeza mapato ya Serikali kupitia huduma zinazotolewa Katika Bandari.
Mbali na kujionea maeneo yao hayo pia wamejionea utayari wa Bandari kavu ya Kwala katika kutoa huduma ambayo imekamilika kwa kwa Asilimia 100 ya Ujenzi wake, ikiwa ni matokeo chanya ya uongozi madhubuti wa Serikali ya awamu ya sita ambayo imewezesha Shilingi Bilioni 83.247 kwa ajili ya kujenga na kuendeleza Bandari hiyo, ikuhusisha pia Ujenzi wa Barabara ya zege yenye urefu wa kilometa 15.5 kutoka Barabara ya Morogoro kuingia na kutoka Bandarini hapo pamoja na miundombinu ya reli mchepuko yenye urefu wa kilometa 1.3 ambayo pia inaingia na kutoka katika Bandari hiyo.
Viongozi hao kutoka Nchi za Burundi na DRC pia ni Wajumbe wa Bodi ya Central Corridor inayoendelea na vikao vyake Jijini Dar es Salaam na katika ziara yao hiyo wameongozana na Balozi mdogo wa DRC hapa nchini Mhe. Louis Manzombi Kisombo, Mwakilishi wa Sekta Binafsi wa DRC Mhe. Mudekereza Namegabe, Viongozi kutoka Wizara ya Uchukuzi wakiongozwa na Mkurugenzi wa Miundombinu ya Uchukuzi Mha. Shomari Shomari aliyemuwakilisha Katibu Mkuu wa Uchukuzi, Naibu Mkurugnzi wa Miundombinu Mha. Christopher Mang’wela na Maafisa kutoka Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari Tanzania( TPA).