

Hongera Rais wa jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt Samia Suluhu Hassan, kwa kutimiza miaka minne ya uongozi wenye mafanikio.

Kamati ya kudumu ya Bunge ya Miundombinu imeipongeza Serikali kwa mabadiliko makubwa ya miundombinu yaliyofanyika katika Bandari ya Dar es Salaam na kuleta tija na ufanisi mkubwa katika kuhudumia Shehena.
Pongezi hizo zimetolewa na Mwenyekiti wa Kamati hiyo Mhe. Selemani Kakoso ( Mb) tarehe 18 Machi 2025, baada ya Kamati kutembelea na kukagua mradi wa maboresho wa Bandari ya Dar es Salaam.
“ Tunaipongeza sana Serikali kwa kazi kubwa na kiwango kikubwa cha mabadiliko kilichofanyika. Tumeona hakuna kuchelewa wala kukwama kwa huduma ya shehena, hakika mafanikio ni makubwa na mapato yameongezeka sana, hakika uwekezaji umelipa.” Amesema Mhe. Kakoso.
Mhe. Kakoso pia ametoa Rai kwa Menejimenti ya TPA kuhakikisha inatenga maeneo makubwa na ya kutosha kwa ajili ya faida ya baadae kwa matumizi ya Bandari kwani mtaji mkubwa kwa maendeleo ya Bandari ni ardhi.
Kwa upande wake Naibu Waziri wa Uchukuzi Mhe. David Kihenzile( Mb) ameishukuru Kamati kwa ziara yao iliyowawezesha kuona kazi kubwa inayofanywa na Serikali katika maboresho makubwa ya miundombinu kwenye Bandari ya Dar es Salaam huku akiihakikishia kamati hiyo kuwa maoni, ushauri na maelekezo waliyoyatoa yatafanyiwa kazi.
Mapema akisoma taarifa ya maboresho ya Bandari ya Dar es Salaam kwa kamati kwa niaba ya Mkurugenzi Mkuu, Naibu Mkurugenzi Mkuu wa TPA Dkt. Baraka Mdima,amesema maboresho ya miundombinu yaliyofanyika katika Bandari ya Dar es Salaam yameleta tija na ufanisi mkubwa katika kuhudumia Shehena Bandarini hapo na hivyo kuchagiza ongezeko la makusanyo ya mapato ya Nchi.
“ Mapato yaliyokusanywa na TPA kwa kipindi cha Julai 2023 hadi Juni 2024, yamefikia Shilingi Trilioni 1.4 na kulingana na taarifa mbalimbali za kiuchumi, mchango wa sekta ya Bandari katika mapato yanayotokana na ushuru wa forodha, yameongezeka kwa asilimia 18, kutoka wastani wa Shilingi Bilioni 850 kwa mwezi hadi kufikia wastani wa Shilingi Trilioni 1.” Amesema Dkt. Mdima.
Pia Dkt. Mdima amesema TPA inathamini na ushirikiano inaoupata kutoka Serikalini, hususani kutoka katika Kamati hiyo na kusisitiza kuwa ushirikiano zaidi unahitajika ili Mamlaka iweze kutekeleza mipango yake inayolenga kuboresha miundombinu na tija katika Bandari zote nchini, ili kuwa chachu ya maendeleo ya Kijamii na Kiuchumi.

Serikali ya Tanzania, kupitia Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari (TPA), imewekeza katika ujenzi wa Bandari Kavu ya Kwala, mradi wa kimkakati unaolenga kuongeza ufanisi wa Bandari ya Dar es Salaam na kuifanya kuwa kitovu bora cha biashara kwa nchi jirani.
Akizungumza na waandishi wa habari leo, Machi 16, 2025, Msemaji Mkuu wa Serikali, Gerson Msigwa, wakati wa ziara yake ya kikazi katika eneo la Bandari Kavu ya Kwala amesema bandari hiyo iliyopo Vigwaza, Kibaha, mkoani Pwani, ni suluhisho la muda mrefu kwa changamoto ya msongamano wa mizigo bandarini.
Ameeleza kuwa moja ya faida kubwa ya Bandari Kavu ya Kwala ni kupunguza muda wa kushughulikia mizigo katika Bandari ya Dar es Salaam kwa kuhifadhi makontena na shehena kubwa ya bidhaa Kwala, ufanisi wa bandari kuu utaongezeka, hivyo wateja kuhudumiwa kwa haraka zaidi.
“Hii itapunguza gharama za ucheleweshaji wa mizigo na kuimarisha mazingira bora zaidi ya biashara na uwekezaji nchini.”
Msigwa amesema bandari hiyo inatarajiwa kuhudumia makasha 823 kwa siku, yakiwemo yanayokwenda nchi jirani. Hii inamaanisha kuwa kwa mwaka itahudumia hadi makasha 300,395, sawa na asilimia 30 ya makasha yote yanayopitia Bandari ya Dar es Salaam.
Aidha, amesema Serikali imewekeza katika miundombinu muhimu ili kuhakikisha ufanisi wa bandari hiyo, ikiwemo ujenzi wa reli ya mchepuko inayounganisha Kwala na Shirika la Reli Tanzania (TRC), barabara za zege, na mtandao wa umeme wa uhakika.
“Kupitia reli, mizigo kutoka Bandari ya Dar es Salaam itaweza kusafirishwa moja kwa moja hadi Kwala, hatua itakayopunguza idadi ya malori barabarani, msongamano, ajali zisizo za lazima na kuokoa barabara zetu,” amesema Msigwa.
Mbali na hayo, Msigwa ameeleza kuwa awamu ya kwanza ya ujenzi wa miundombinu ndani ya eneo la mradi imekamilika kwa asilimia 80.
“Shughuli hizo zinahusisha na Mtandao wa barabara za zege zinazoweza kubeba malori ya mizigo, Jengo la kituo cha kupambana na moto, Jengo la utawala litakalohifadhi ofisi za mashirika ya serikali na watoa huduma za kitaalamu, Mfumo wa maji ya mvua, Mtandao wa umeme na maji safi, Hifadhi za viwanda zenye jumla ya mita za mraba 26,000 na Lango kuu na malazi ya wafanyakazi.”
Kadhalika Msigwa amesema bandari hiyo itakapokamilika, itakuwa na viwanda vikubwa na vya kati 200 pamoja na viwanda vidogo 300 vinavyohusika na Usindikaji wa vyakula, Utengenezaji wa vifaa, Viwanda vya dawa, Vifaa vya ujenzi, Usindikaji wa viatu na nguo, pamoja na Viwanda vya kemikali.
Kwa upande wa Kongani ya viwanda ya SINO-TAN, Msigwa amesema kuwa kongani hiyo itaongeza ajira kwa Watanzania ambapo inatarajiwa kutoa zaidi ya ajira za moja kwa moja 100,000 na ajira zisizo za moja kwa moja 500,000. Mradi huu unajengwa kwa awamu tano.
Amesema hadi sasa, viwanda vitatu tayari vimeanza uzalishaji, vingine vitatu vipo katika hatua za mwisho za kufunga mitambo, na viwanda vinne vinatarajiwa kuanza ufungaji wa mitambo ifikapo mwisho wa Aprili 2025.
Mwisho

Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari Tanzania (TPA) imepongezwa kwa kuweka mikakati ya kuwajengea uwezo Watumishi wanawake ili waweze kufanyakazi na kuleta matokeo chanya kwa Taasisi na Taifa kwa ujumla.
Hayo yamesemwa na Naibu Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania (BoT) ,Uthabiti na Usimamizi wa Sekta ya Fedha Bi.Sauda Msemo katika hafla ya maadhimisho ya siku ya Wanawake Duniani iliyoandaliwa na Wanawake watumishi wa TPA na kufanyika katika jengo la Makao Makuu ya TPA jijini Dar es Salaam Machi 15,2025.
Katika salamu zake za ukaribisho Mkurugenzi wa Rasilimali Watu na Utawala Bw.Mbarikiwa Masinga kwa niaba ya Mkurugenzi Mkuu wa TPA,amewataka Watumishi wanawake kufanyakazi kwa kushirikiana na kupendana bila kuwekeana chuki ili kufikia malengo makubwa ya Taasisi.
Awali akizungumza wakati akiwakaribisha wageni waalikwa katika hafla hiyo, Meneja Rasilimali Watu wa Bandari ya Dar es Salaam Bi.Mwajuma Mkonga amesema walizindua siku ya Wanawake Duniani kwa kupima afya za wafanyakazi na familia zao katika kituo cha afya kilichopo Bandarini na kutoa misaada ya vifaa tiba vyenye thamani ya shilingi milioni 49 na kwamba TPA imekuwa ikifanya hivyo kwa miaka minne mfululizo.
Katika kuadhimisha siku ya Wanawake Duniani Wanawake watumishi wa TPA walitoa misaada ya vifaa tiba katika hospitali za Wilaya ya Kigamboni vyenye thamani ya shilingi milioni 24 na hospitali ya Rufaa ya Temeke vyenye thamani ya shilingi milioni 25.
Pia katika kuadhimisha siku hiyo wameandaa Tuzo za Mabadiliko Chanya,mwanamke aliyebuni kitu kilicholeta mabadiliko na kuleta tija kwenye Taasisi.
Katika kuadhimisha siku ya Wanawake Duniani,Watumishi wanawake wa Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari Tanzania (TPA) wamebuni shindano la kugombea Tuzo ya Mabadiliko chanya, mchakato uliohitimishwa kwenye halfa iliyofanyika katika ukumbi wa jengo la Makao Makuu wa One Stop Centre jijini Dar es Salaam, Machi 15,2025.
Jaji wa Tuzo hizo Bi.Rosemary Ndesamburo alimtangaza Bi.Lucy Kalinga kuwa mshindi wa tuzo hizo zilizoanza kwa mara ya kwanza mwaka huu huku Bi. Farida Ismaili Hamisi alijinyakulia nafasi ya pili na Bi.Salma Kitwana akipata nafasi ya tatu.
- MENEJIMENTI YA TPA YAPOKEA UGENI WA WAZIRI WA NCHI, MASHAURI YA KIGENI NA BIASHARA MHE. NAELE RICHMOND
- KAMATI YA KUDUMU YA BUNGE YA MIUNDOMBINU IMERIDHISHWA NA UTENDAJI KAZI WA TPA KATIKA BANDARI YA TANGA
- HONGERA KWA MHE. BALOZI NA MKUU WA JESHI LA POLISI MSTAAFU KWA KUTEULIWA TENA KUWA MWENYEKITI WA BODI YA WAKURUGENZI YA TPA
- WATUMISHI WA TPA WASHIRIKI KUTOA MISAADA YA VIFAA VYA TIBA KATIKA HOSPITALI ZA WILAYA YA KIGAMBONI NA TEMEKE