Mjumbe wa Halmashauri Kuu ya Taifa ya Chama Cha Mapinduzi (MNEC) Comrade Richard Kasesera,tarehe 3 Februari, 2026 ameongoza ujumbe wa Wanachama wa CCM katika ziara ya kikazi ya kutembelea Bandari ya Mtwara.
Lengo la ziara hiyo ni kujionea maendeleo ya Bandari ya Mtwara baada ya maboresho mbalimbali yaliyofanywa na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania pamoja na kupata taarifa ya utendaji kazi wa Bandari.
Katika ziara hiyo, Kaimu Meneja wa Bandari ya Mtwara Kapt. Paul Muchwampaka alieleza masuala mbalimbali ikiwemo mafanikio yaliyopatikana pamoja na changamoto kadhaa zinazoikabili Bandari ya Mtwara.
Baada ya kupokea taarifa hiyo, Comrade Kasesera alipongeza utendaji kazi mzuri wa Bandari ya Mtwara ikiwa ni pamoja na uwezo mkubwa wa kuhudumia shehena. Aidha, alieleza kuwa atawasilisha katika ngazi za juu masuala mbalimbali ikiwemo changamoto zilizopo ili zitafutiwe ufumbuzi wa haraka kwa lengo la kuendelea kuimarisha ufanisi na mchango wa Bandari ya Mtwara katika maendeleo ya Taifa.
Maafisa wanafunzi na Wakufunzi wa Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) kutoka Chuo cha Mafunzo ya Kikosi Maalum kilichopo Sangasanga Wilaya ya Morogoro leo tarehe 3 februari 2026 wametembelea Bandari ya Dar es Salaam ambapo pamoja na mambo mengine wamejifunza shughuli za Bandari pamoja na namna TPA ilivyojidhatiti na utayari wake katika kupambana na hatari za kiusalama katika Bandari zake hususan Bandari ya Dar es Salaam ambalo ni langu kuu la Biashara kitaifa na kimataifa.
Ziara hiyo imeongozwa na Meneja Ulinzi na Usalama Bw. Said J. Mollel Kwa niaba ya Kaimu Mkurugenzi wa Bandari ya Dar es Salaam Bw. Abed G. Abed.


Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari Tanzania (TPA), Bw. Plasduce Mkeli Mbossa, amewataka watumishi wapya wa taasisi hiyo kuweka maslahi ya umma mbele ya maslahi binafsi na kuutumikia umma kwa uadilifu, uwazi na uwajibikaji ili kulinda imani ya wananchi kwa Serikali.
Akizungumza wakati wa kufungua kozi ya awali ya mafunzo kwa watumishi wapya (Induction Course) iliyofanyika Makao Makuu ya TPA jijini Dar es Salaam, tarehe 2 Februari,2026, Bw. Mbossa amesema Serikali inawatazamia watumishi wa umma kuwa mabalozi wa mabadiliko chanya ndani ya taasisi zao na katika jamii kwa ujumla.
Alisisitiza kuwa utumishi wa umma si ajira ya kawaida, bali ni wito wa kulitumikia taifa kwa uaminifu na uzalendo wa dhati, akiwahimiza watumishi wapya kuzingatia maadili ya kazi, kufanya kazi kwa weledi na kujenga utamaduni wa uwazi na uwajibikaji katika utekelezaji wa majukumu yao ya kila siku.
“Kumbukeni kuwa imani ya wananchi kwa Serikali hujengwa au hubomolewa kupitia mwenendo wa watumishi wake,” alisema Bw. Mbossa, akionya dhidi ya vitendo vinavyoweza kuhatarisha taswira ya taasisi na utumishi wa umma kwa ujumla.
Aidha, aliwahimiza watumishi wapya kutumia mafunzo waliyoyapata kama msingi wa kujenga taaluma zao, wakizingatia misingi ya uadilifu, weledi na uzalendo, sambamba na kuwa sehemu ya suluhisho la changamoto badala ya kuwa chanzo cha matatizo.
Akihitimisha hotuba yake, Mkurugenzi Mkuu aliwatakia watumishi wapya mafunzo mema na safari njema katika utumishi wa umma, akisisitiza umuhimu wa kulinda heshima ya taasisi na Taifa kwa ujumla.
Kozi hiyo ya “induction” inalenga kuwaandaa watumishi wapya wa TPA kwa kuwajengea uelewa wa majukumu ya taasisi, misingi ya utumishi wa umma, maadili ya kazi na matarajio ya Serikali katika kuboresha ufanisi wa bandari na kuchangia maendeleo ya uchumi wa Taifa.



Chama cha Wafanyakazi wa Shughuli za Meli na Bandari (DOWUTA) tawi la Makao Makuu, kimekamilisha mchakato wa Uchaguzi wa nafasi mbalimbali za chama hicho Januari 30,2024.
Katika uchaguzi huo uliokuwa na hamasa kubwa tofauti na miaka iliyopita,ambapo mshindi wa nafasi ya Mwenyekiti ni Bw.Felician Hasunga na Bw. Isaac Mtamba akiibuka mshindi katika nafasi ya Katibu Mkuu.
Nafasi zingine zilizokuwa zinagombaniwa ni nafasi ya Uwakilishi wa Vijana wanaume ambapo Bw. Shamte Luwali na Bw. Omary Khalid walifungana kwa kulingana idadi ya kura na hivyo uchaguzi wa nafasi hiyo itarudiwa, huku kwa upande wa Vijana wanawake mshindi ni Bi. Hilda Shundi.
Nafasi tano Wajumbe wanawake washindi ni Bi. Irene Mmari, Bi. Mary Mahinya, Bi. Queen Chiwanga, Bi. Caroline Urio na Bi. Mariam Namota.
Washindi wa nafasi za uwakilishi wa idara ni Bw. Zubeir Sungura, Bw. Aloyce Kakusa, Bi. Esther Mchomvu, Bw. Calist Nyaki, Bw. Atufigwegwe Mwanjala, Bw. Mutasa na nafasi ya mweka hazina wa chama imechukuliwa na Bw. Adili Mindolo.



Wafanyakazi wa Bandari ya Tanga wamemchagua Bw. Aliko Mwakipagala kuwa Mwenyekiti wa Chama cha Wafanyakazi wa Shughuli za Meli na Bandari (DOWUTA) tawi la Tanga, huku Bw. Iddi Mfaume Bode akichaguliwa kuwa Katibu wa tawi hilo.
Pia katika Mkutano huo wa uchaguzi, Wafanyakazi waliwachagua wawakilishi mbalimbali kuunda Kamati ya Utendaji ya DOWUTA tawi la Bandari ya Tanga.
Aidha akifungua mkutano huo wa uchaguzi, Meneja wa Bandari ya Tanga, Bw. Salehe Mbega, alitoa rai kwa wafanyakazi wa Bandari ya Tanga kuendelea kufanya kazi kwa bidii ili kuhakikisha ufanisi unaendelea kunapatikana katika bandari hiyo.
Akiongea katika Mkutano huo Bw. Mbega amesema, ufanisi unaoonekana katika bandari hiyo ni pamoja na utendajikazi uliotukuka kutoka kwa wafanyakazi hivyo, aliwataka kuendelea kufanya kazi kwa bidii ili tuendelee kuvuka malengo ya kila mwaka yanayotolewa na serikali.
“Bandari ya Tanga imeendelea kuvutia wadau mbalimbali kutaka kufanyakazi na sisi hii yote ni kutokana na tunavyofanya kazi vizuri hivyo nawaomba tuendelee kuwajibika ipasavyo ili mwisho wa siku tufaidike kwa kujituma kwetu”. Aliongeza Bw. Mbega
Aidha Bw. Mbega aliwahakikishia wafanyazi hao changamoto zote zitaendelea kufanyiwa kazi kuhakikisha zinapatiwa ufumbuzi ikiwa ni pamoja na kuendelea kuboresha maslahi.
Katika hatua nyingine Bw. Mbega aliwatakia heri wanachama na wagombea wote waliotia nia katika uchaguzi huo na kuwataka kwenda kusimamia maslahi ya wafanyakazi pamoja na mambo muhimu yaliwekwa kwa kuzingatia sheria na kanuni za utumishi.
Awali akimkaribisha Meneja huyo, Mwenyekiti wa muda wa DOWUTA Tawi la Tanga aliyekuwa anamaliza muda wake Bw. Aliko Mwakipagala alimhakikishia Bw. Mbega kuwa chama hicho kitaendelea kutoa ushirikiano kwa uongozi wa bandari ili kuhakikisha malengo katika uhudumiaji wa shehena yanafanikiwa.
Katika kipindi cha kwanza Mwakipagala alishikia nafasi ya Mwenyekiti baada ya aliyekuwa Mwenyekiti Bw. Ali Sankole kustaafu utumishi wake bandarini.



EN
SW
FR
TPA ChatBot - "Nahodha"