Select your language

Mkuu wa Wilaya ya Tanga, Mhe. Dadi Kolimba amewapongeza Watumishi wa Bandari ya Tanga na kuwataka waendelee kufanya kazi kwa bidii ili kuunga mkono juhudi za Serikali katika uwekezaji mkubwa uliofanyika katika bandari hiyo.

Mhe. Kolimba ametoa pongezi hizo baada ya kutembelea na kukagua banda la Bandari ya Tanga kwenye maonesho ya 12 ya Biashara na Utalii  (Tanga Trade Fair) yanayofanyika katika viwanja vya Mwahako  kuanzia tarehe 28 Mei hadi 6 Juni 2025.

“Serikali imewekeza kiasi cha Shilingi Billioni 429.1 hivyo endeleeni kuwajibika ipasavyo ili uwekezaji huo uweze kuzaa matunda sambamba na uhudumiaji wa shehena na ukusanyaji wa mapato uzidi kuongezeka”. Alisema Kolimba.

Awali akitoa maelezo kwa  Mkuu wa Wilaya huyo, Kaimu Mkuu wa Idara ya Usaidizi wa Biashara Bi. Rose Tandiko kwa niaba ya Meneja wa Bandari ya Tanga, amesema ushiriki wa Bandari ya Tanga katika maonesho hayo ni kutoa elimu kwa umma juu ya faida inayopatikana baada ya mradi wa maboresho ya Bandari kukamilika sambamba na kuunga mkono juhudi za Serikali  katika shughuli mbalimbali za kukuza biashara na Utalii za Mkoa huo.

Pia Bi. Tandiko ametoa rai kwa wafanyabiashara kuitumia Bandari ya Tanga kwani imeboresha huduma zake na hakuna msongamano kutokana na utendaji kazi wenye ufanisi na wafanyakazi wenye ari kubwa.

Aidha Bi Tandiko amesema uwekezaji uliofanywa na Serikali ulikuwa na lengo la kuijengea uwezo bandari hiyo ili iweze kuhudumia shehena kutoka tani 750,000 hadi tani 3,000,000 kwa mwaka.

Maonesho ya 12 ya Biashara na Utalii ambayo husimamiwa na Chemba ya Biashara , Viwanda na Kilimo Tanzania (TCCIA ) ambapo kauli mbiu mwaka huu ni  “Mwonekano wa Wadau Sekta ya Umma na Binafsi Kwenye Uwekezaji, Ukuaji na Uendelevu wa Biashara”.