

Mwandishi Wetu
Jumuiya ya Wafanyabiashara Tanzania (JWT) imeipongeza Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari Tanzania (TPA) kwa kuendelea kuboresha huduma zake katika Bandari zake na kufanya Wafanyabiashara kuendelea kufurahia huduma na kuendelea kutumia bandari za TPA.
Pongezi hizo zimetolewa tarehe 25 Novemba,2024 kupitia Risala yao iliyosomwa na Mwenyekiti wa Jumuiya hiyo kanda ya Ziwa Victoria Bw. Nicholaus Basimaki, katika Mkutano wa 10 wa mwaka 2024, uliofanyika Ukumbi wa Ubungo Plaza Jijini Dar es Salaam.
TPA ilikuwa ni miongoni mwa Wadhamini wa Mkutano huo wa siku moja umeshirikisha Wajumbe 400 kutoka Tanzania Bara na Zanzibar.

Na Mwandishi Wetu
Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari Tanzania (TPA) imezihakikishia Nchi zinazohudumiwa na Bandari za Tanzania chini ya TPA kuwa, itaendelea kuunga mkono juhudi na jitihada za kuimarisha biashara ya kikanda na kukuza uchumi.
Akizungumza kwa niaba ya Mkurugenzi Mkuu wa TPA katika ufunguzi wa Mkutano wa tano wa Juma la Shughuli za Kibandari na Forodha “Ports & Customs Week 2024“uliofanyika tarehe 3 hadi 4 Desemba,2024 Jijini Dar es Salaam, Mkurugenzi wa Masoko na Uhusiano Dkt. George Fasha, amesema nia hiyo ya TPA inaenda sambamba na ukuaji wa maendeleo ya teknolojia pamoja na matokeo chanya kwa Bandari na mifumo ya forodha na kuimarisha ushirikiano ili kuendeleza na kuwezesha biashara na kukuza uchumi miongoni mwa nchi zinazotumia Bandari za Tanzania.
Mkutano huu wa Shughuli za Kibandari na Forodha ni muhimu kwani unatoa suluhu za kiteknolojia kwa changamoto zinazokabili bandari na mamlaka ya forodha barani Afrika ukiwa unaongozwa na kaulimbiu ya “Kuimarisha Ushirikiano wa Kikanda na Uwekaji mifumo ya Kidijiti wa Mipaka, Bandari na Forodha.

Na Mwandishi Wetu
Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari Tanzania (TPA) Bw. Plasduce Mbossa amesema kuwa wamejipanga kufanya upanuzi wa Bandari za Mamlaka ili kuendelea kutoa huduma shindani katika soko la Afrika na Kimataifa.
Akizungumza hivi karibuni, Mbossa amesema kuwa TPA imejiweka katika nafasi nzuri zaidi ya kiushindani kutokana na uwekezaji wake unaoendelea katika bandari mbalimbali hapa nchini.
Moja ya mikakati hiyo ni pamoja na mpango wa kupanua na kujenga gati 10 katika Bandari ya Dar es Salaam ili kuongeza ufanisi na tija katika bandari hiyo.
“Katika kuhakikisha wateja wetu wanaendelea kupata huduma bora na stahiki sisi kama mamlaka tumekuja na mpango wa kuongeza gati 10 katika bandari ya Dar es salaam,”
“Hii inaenda kupanua soko la biashara kwa watumiaji wa bandari yetu kwani ufanisi utakuwa ni mkubwa na utakidhi mahitaji ya wateja wetu”, amesema.
Aliongeza kusema TPA imeendelea kuboresha miundombinu ya bandari zake ambazo ni pamoja na bandari ya Bagamoyo, Bandari ya Tanga, Mtwara, Mbamba Bay na bandari zingine ambazo ziko chini ya mamlaka hiyo.
Amesema hayo yote yanafanyika ili kuhakikisha kuwa TPA inachochea uchumi wa Taifa kupitia Bandari zake kwa kushirikiana na wawekezaji waliopo.
“TPA tumejipanga kuufungua uchumi wa Taifa kwa kutumia bandari zetu na ndio maana tumeendelea kuboresha maeneo mengi ya bandari zetu ili ziweze kutoa huduma kwa wateja wetu wa ndani na nje ya nchi.”
“Kwa kupitia uwekezaji ambao tumeufanya katika bandari zetu, matunda yake tumeanza kuyaona ambapo hadi sasa kumekuwa na utofauti mkubwa katika huduma za bandari ukilinganisha na miaka kadhaa ya nyuma”
“Hii inatokana na juhudi za Serikali ya Rais Samia Suluhu Hassan ya kuleta mageuzi makubwa ya kiutendaji katika bandari zetu ili kuchochea biashara zaidi na kukuza uchumi wa nchi yetun”amesema Bw. Mbossa.

Na Mwandishi Wetu
Ili kuendana na malengo ya Uchumi wa Bluu na Bandari ya Kijani (Blue Economy and Green Port), Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari Tanzania (TPA) imeeleza hatua madhubuti inazochukua kuhakikisha kuwa shughuli za kibandari haziathiri mazingira.
Akizungumza wakati wa Kongamano na Maonesho ya Tisa ya Kitaifa ya Sayansi, Teknolojia na Ubunifu (STICE), yanayoendelea katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNICC), Dkt. Olivary John kutoka Chuo cha Bandari alieleza kuwa TPA imechukua hatua tano muhimu kudhibiti uharibifu wa mazingira unaosababishwa na shughuli za kibandari.
Kwa mujibu wa Dkt. Olivary, hatua hizo ni pamoja na kuanzishwa kwa Sera ya Usimamizi wa Mazingira ya TPA, ambayo inatoa mwongozo wa kulinda na kuhifadhi mazingira katika shughuli za bandari. Hatua nyingine ni uwekaji wa vitunza taka katika maeneo mbalimbali ya bandari ili kuhakikisha taka zinakusanywa na kusimamiwa ipasavyo.
Aidha, TPA imeimarisha juhudi za kudhibiti uzalishaji wa taka, ikiwemo kupunguza taka zinazozalishwa kupitia mbinu endelevu. Pia, mamlaka hiyo inazingatia mfumo wa utunzaji wa mazingira kulingana na kanuni za ISO, kuhakikisha bandari zake zinakidhi viwango vya kimataifa vya mazingira.
Hatua ya tano, kwa mujibu wa Dkt. Olivary, ni utunzaji wa bahari na upunguzaji wa uchafuzi wa mazingira kwa kuondoa taka laini na ngumu katika maeneo ya bahari, ili kuhifadhi usafi na uhai wa viumbe wa majini.
Hatua hizi zinathibitisha dhamira ya TPA katika kufanikisha maendeleo endelevu kupitia ulinzi wa mazingira na kuhakikisha bandari zake zinachangia uchumi wa taifa bila kuathiri mazingira.

Na Mwandishi Wetu
Mpango wa uboreshaji miundombinu katika Bandari ya Mtwara unaotekelezwa kupitia Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, umeongeza ufanisi ambapo zaidi ya tani 100,000 za korosho zimesafirishwa katika msimu huu wa zao hilo.
Mafanikio hayo yamepatikana baada ya kuongezwa vifaa vya kupakia na kushusha mizigo, hivyo kuchangia ongezeko la idadi ya meli zinazotia nanga kwenye bandari hiyo hali inayotajwa kuchochea zaidi uchumi katika ukanda wa kusini.
Akizungumza mkoani Mtwara wakati wa ziara ya kukagua maboresho katika bandari hiyo, Waziri wa Uchukuzi Profesa Makame Mbarawa, alisema serikali inatekeleza mkakati huo wenye lengo la kukuza uchumi na kufungua fursa za ajira kwa wananchi.
"Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan amekuwa mstari wa mbele kuweka msukumo kwenye usimamizi na ujenzi wa miundombinu mbalimbali katika sekta ya uchukuzi na ndiyo sababu meli zimeanza kuja kwa wingi," alieleza.
Profesa Mbarawa alibainisha kuwa kabla ya maboresho hayo bandari hiyo ilikuwa kwa siku ikipokea wastani wa meli moja, lakini sasa meli nyingi zaidi zimekuwa zikitia nanga.
"Leo kuna meli zipo zinapakia mizigo, moja ni ya tani 9,000 na nyingine ni tani 30,000. Kesho zitakuja meli zingine tatu zitakazofanyakazi kwa wakati mmoja. Vitendea kazi vimeongezeka zaidi na vingine vitaletwa hapa kutoka Bandari ya Dar es Salaam ambako mwekezaji ameleta mitambo mingine," alisisitiza.