Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC) imeipongeza Menejimenti ya Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari Tanzania ( TPA) kwa usimamizi mzuri wa matumizi ya Fedha za Maboresho yanayoendelea kufanyika kupitia mradi wa maboresho ya Bandari ya Dar es Salaam (DMGP)
Akizugumza tarehe 30 Machi 2025, mara baada ya kumaliza ziara ya kukagua na kutembelea mradi wa maboresho ya Bandari ya Dar es Salaam, Mwenyekiti wa PAC , Mhe.Naghenjwa Kaboyoka (Mb) amesema kamati yake imejiridhisha na usimamizi mzuri wa Mradi huo na Fedha za Umma zimetumika vyema na kufikia malengo yakiyokusudiwa.
“ Kamati imejiridhisha na kazi nzuri iliyofanyika katika Bandari ya Dar es Salaam, kazi yetu kubwa ni kuangalia Kama Fedha za Umma zimetumika vizuri kwa manufaa ya nchi yetu na katika hili Kamati inampongeza sana Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi, Menejimenti ya TPA na Wafanyakazi wote kwa kazi nzuri iliyofanyika hapa.’ Amesema Mhe. Kaboyoka.
Akijibu hoja za Wajumbe wa Kamati hiyo, Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi ya TPA, Mhe. Balozi na IGP Mstaafu Ernest Mangu, ameishukuru Kamati kwa kufanya ziara yao iliyowawezesha kuona hatua iliyofikiwa na thamani ya mradi wa DMGP, huku akiihakikishia kamati hiyo kuwa maelekezo, maoni na ushauri wao utafanyiwa kazi.
Mapema akisoma taarifa ya mradi wa maboresho ya Bandari ya Dar es Salaam (DMGP) mbele ya kamati kwa niaba ya Mkurugenzi Mkuu Bw. Plasduce Mbossa, Naibu Mkurugenzi Mkuu wa TPA Dkt. Baraka Mdima, amesema hadi sasa kukamilika kwa utekelezaji wa mradi katika baadhi ya maeneo kumeleta manufaa mbalimbali ikiwemo kuongezeka kwa uwezo wa Bandari ya Dar es Salaam kuhudumia Meli kubwa zenye kubeba makasha hadi 8,000, kuongezeka uwezo wa kuhudumia shehena kutoka tani milioni 16 hadi tani milioni 28 kwa sasa na kuongeza uwezo wa kiushindani kati ya Bandari ya Dar es Salaam na Bandari nyingine.

Mradi wa maboresho ya Bandari ya Dar es Salaam (DMGP) unagharimu Shilingi Trilioni 1.118 ambazo ni Fedha za mkopo kutoka Benki ya Dunia, Fedha za msaada kutoka kwa Wafadhili na mapato ya ndani ya TPA.
Mradi huu umehusisha kuimarisha Gati na 1-7 na kuongeza kina kutoka mita 8 hadi mita 14.5 na kujenga Gati maalum ( RoRo Berth) la kuhudumia meli za magari, kuongeza kina na Upana wa lango la kuingilia Meli na eneo la kugeuzia Meli , kuimarisha Gati na 8-11 na kuongeza kina kutoka mita 12 hadi kufikia kina cha mita 14.5, kuboresha mtandao wa Reli ndani ya Bandari na kusimika Mfumo wa Umeme Bandarini.

Wadau wa sekta ya Uchukuzi wanaoshiriki Mkutano wa pili wa Uchukuzi na Usafirishaji - East Africa Cargo Connect Summit Jijini Dar es Salaam, wametakiwa kuutumia Mkutano huo kuwa na majadiliano yenye faida na yenye kuleta maazimio chanya yatakayoleta mchango mkubwa wenye kuongeza tija na ufanisi katika shughuli za uchukuzi zikiwemo za kibandari.
Kauli hiyo imetolewa tarehe 27 Machi, 2025 na Mkurugenzi wa Masoko na Uhusiano wa TPA Dkt. George Fasha aliyewakilishwa na Afisa Masoko Mkuu Bi. Fatma Adadi Rajab ambaye amesema majadiliano yenye tija ni muhimu kwani mkutano huo unaonyesha nia ya dhati ya Wadau wa Uchukuzi katika kuiboresha sekta hiyo na kuhakikisha utoaji huduma unaendelea kuwa bora zaidi.
Mkutano huo wa siku moja ni jukwaa la kuwakutanisha pamoja Wadau wa sekta ya uchukuzi kwa njia ya maji, anga, reli na barabara, kujadaliana pamoja changamoto zinazowakabili na utatuzi wake pamoja na kufungua fursa mpya za uwekezaji kupitia sekta hiyo na kuikuza zaidi.
Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari Tanzania (TPA) imedhamini Mkutano huo ulioshirikisha Wadau wa Uchukuzi kutoka nchi za Afrika Mashariki, Jumuiya ya maendeleo kusini mwa Afrika ( SADC) na nchi za Afrika magharibi.
Tuzo mbalimbali za umahiri zimetolewa katika Mkutano huo ikiwemo Tuzo ya “The Tanzania Maritime Visionary Leadership Award” iliyotolewa kwa Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari Tanzania ( TPA) Bw. Plasduce Mkeli Mbossa kwa kutambua na kuthamini Uongozi wake wenye maono katika sekta ya uchukuzi wa njia ya maji hapa nchini.

Bandari ya Mtwara imeendelea kupongezwa kwa ufanisi mkubwa wa kuhudumia shehena mbalimbali ikiwemo shehena zenye kemikali.
Pongezi hizo zimetolewa tarehe 25 Machi, 2025 na Mwakilishi wa Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi wa Mamlaka ya Maabara ya Mkemia Mkuu wa Serikali Tanzania Profesa Said Vuai, kufuatia Bodi hiyo kufanya ziara katika Bandari ya Mtwara ambapo imeshuhudia shughuli mbalimbali za utekelezaji zikiendelea.
Kaimu Meneja wa Bandari ya Mtwara Bw. Mtunze Mwarabu Sudi amesema Bandari hiyo imeendelea kushirikiana vema na Ofisi ya Maabara ya Mkemia Mkuu wa Serikali katika kutekeleza shughuli mbalimbali za kuhudumia shehena.

Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma (PIC) imemuelekeza Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi ya Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari Tanzania (TPA) na Menejimenti yake kuendelea kumsimamia ipasavyo Mkandarasi anayetekeleza mradi wa maboresho na upanuzi wa Bandari ya Mwanza Kaskazini ili aweze kukamilisha mradi huo kwa wakati na kwa kiwango kulingana na thamani ya fedha.
Akizungumza Machi 21, 2025 Jijini Mwanza baada ya kutembelea na kukagua mradi huo, Mwenyekiti wa Kamati hiyo Mhe. Augustine Vuma (Mb),amesema kukamilika kwa wakati kwa mradi huo ni hatua muhimu katika kuboresha hali ya usafiri na usafirishaji ndani ya Ziwa Viktoria.
“ Kwa ujumla Sekta ya Bandari Mhe. Rais ametoa fedha nyingi sana na kwa hili tunampongeza sana kwa uamuzi wake huu maana tunaona miradi mingi ya maboresho na ujenzi wa bandari pamoja na ukarabati na ujenzi wa Meli. Kwa ujumla TPA mnafanya kazi nzuri na tunawapongeza kwa mradi huu mzuri na wa kimkakati, muhimu ni usimamizi makini ili mapato yaongezeke na tija ionekane.” Amesema Mhe.Vuma
Pia ameiagiza TPA kuhakikisha inaendeleza ushirikiano na Sekta Binafsi ili kuongeza ufanisi zaidi katika Bandari na kuendelea kuimarisha maeneo ya pembezoni kupitia Bandari.
Akijibu hoja za Wajumbe wa Kamati, Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi ya TPA, Mhe. Balozi na IGP Mstaafu Ernest Mangu, ameishukuru Kamati kwa ziara yao iliyowawezesha kuona mradi wa maboresho na upanuzi wa Bandari ya Mwanza Kaskazini, huku akiihakikishia kamati hiyo kuwa maoni, ushauri na maelekezo waliyoyatoa yatafanyiwa kazi.
Mapema akisoma taarifa ya mradi wa maboresho na upanuzi wa Bandari ya Mwanza Kaskazini mbele ya kamati kwa niaba ya Mkurugenzi Mkuu Bw. Plasduce Mbossa, Naibu Mkurugenzi Mkuu wa TPA Dkt. Baraka Mdima,amesema kukamilika kwa maboresho na upanuzi wa Bandari hiyo kutaenda sambamba na mabadiliko ya kisasa ya Teknolojia katika kuendesha Bandari na kutoa huduma za kiwango cha kisasa zaidi ikiwa ni pamoja na kuongeza tija na ufanisi mkubwa katika kuhudumia Shehena.
Mradi wa maboresho na upanuzi wa Bandari ya Mwanza Kaskazini unagharimu shilingi Bilioni 18.6, ikiwa ni jitihada za Serikali kupitia Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari Tanzania ( TPA) katika kuboresha hali ya usafiri na usafirishaji ndani ya Ziwa Viktoria.

Baraza Kuu la Wafanyakazi wa Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari Tanzania ( TPA) leo tarehe 19 Machi 2025, limefanya kikao chake cha Thelathini na Saba (37) mjini Bagamoyo Mkoa wa Pwani, kinacholenga kujadili na kuthibitisha Mapendekezo ya mpango wa Bajeti ya Mamlaka kwa mwaka wa Fedha 2025/ 2026 pamoja na Kupitia na kuthibitisha Kumbukumbu za Kikao cha Thelathini na Sita (36) kilichofanyika tarehe 2 - 3 Oktoba,2024.
Baraza hilo limeongozwa na Naibu Mkurugenzi Mkuu wa TPA Dkt. Baraka R. Mdima ambapo awali Baraza hilo lilitanguliwa na Kikao cha Kamati ya Utendaji ya Baraza kuu la Wanyakazi kilichoongozwa na Mkurugenzi wa Rasilimaliwatu na Utawala Bw. Mbarikiwa Masinga kwa niaba ya Naibu Mkurugenzi Mkuu wa TPA Dtk. Baraka R. Mdima.

- SERIKALI ZA BURUNDI NA YA KONGO (DRC) YAIPONGEZA SERIKALI YA TANZANIA KWA KUIMARISHA BANDARI KAVU YA KWALA
- FOUR YEARS OF HER EXCELLENCY, PRESIDENT DR. SAMIA SULUHU HASSAN IN THE OFFICE
- MIAKA MINNE YA UONGOZI MADHUBUTI
- KAMATI YA KUDUMU YA BUNGE YA MIUNDOMBINU IMERIDHISHWA NA UTENDAJI KAZI WA TPA KATIKA BANDARI YA DAR ES SALAAM
EN
SW
FR
TPA ChatBot - "Nahodha"