Naibu Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi (Sekta ya Uchukuzi), Mhe. Atupele Mwakibete amekagua maendeleo ya ujenzi wa Bandari Kavu ya Kwala ili kuona kama ipo tayari kuanza kutoa huduma. Kukamilika na kuanza kutoa huduma kwa bandari hiyo, kutaongeza ufanisi na kuchochea kukua zaidi kwa shehena inayohudumiwa katika Bandari ya Dar es Salaam. Mbali ya kuchochea ukuaji wa shehena na kuongeza ufanisi, kukamilika kwa bandari hiyo pia kutasaidia kupunguza msongamano wa mizigo katika Bandari ya Dar es Salaam na kuongeza mapato ya Serikali kupitia huduma zitakazokuwa zikitolewa bandarini hapo. Kukamilika kwa ujenzi wa Bandari ya Kwala ni matokeo chanya ya uongozi wa Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Mhe Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt, Samia Suluhu Hassan ambayo imewezesha ujenzi huo kwa kuidhinisha kiasi cha TZS 83.247 Bilioni kutumika kwa ajili ya ujenzi wa bandari hiyo. Mradi wa Bandari hiyo unahusisha ujenzi wa Barabara ya zege yenye urefu wa Kilometa 15.5 kutoka Mzani wa Vigwaza hadi kuingia Bandarini pamoja na ujenzi wa miundombinu ya reli mchepuko yenye urefu wa kilometa 1.3